1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Auwawa kwa kupigwa risasi uwanja wa ndege wa Orly

18 Machi 2017

Vikosi vya usalama vimemuuwa kwa kumpiga risasi mwanaume mmoja aliyejaribu kuikwapuwa bunduki ya askari katika uwanja wa ndege wa Orly,Paris na kulazimisha kuondolewa kwa watu katika uwanja huo wenye harakati kubwa.

https://p.dw.com/p/2ZU5v
Frankreich Flughafen Paris Orly, Angreifer auf Soldaten erschossen
Picha: Reuters/B. Tessier

Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 39 alietambulika kama Muislamu aliepandikizwa itikadi kali ambaye alikuwa akifuatiliwa na polisi na mashirika ya kijasusi nchini humo Jumamosi (18.03.2017)awali alimpiga risasi na kumjeruhi afisa mmoja wa polisi kufuatia ukaguzi wa kawaida wa usalama bararani kaskazini mwa Paris.

Wakati nchi hiyo ikiwa katika kampeni kali ya uchaguzi kufuatia miaka miwili ya mashambulizi dhidi ya raia kwa kuyalenga maeneo ya mkusanyiko wa umma yaliofanywa na kundi linalojiita Dola la Kiislamu mengi yakitokea katika mji wa Paris kumepelekea mwendesha mashtaka kuanzisha uchunguzi.

Duru ya polisi imemtambulisha mtu huyo kuwa Zied B na kwamba alikuwa akijulikana na polisi kwa vitendo vyake vya wizi na makosa ya madawa ya kulevya.Msemaji wa jeshi amesema aliuwawa kwa kupigwa risasi baada ya kushindana na askari wa kike katika ukumbi wa uwanja wa ndege baada ya awali kumpiga risasi na kumjeruhi afisa wa polisi wakati wa ukaguzi wa polisi barabarani upande wa pili wa Paris.

Baba na kaka wa mwanaume huyo wako kizuizini polisi.Kituo cha televisheni cha BFM bila ya kutaja chanzo chake kimesema mshambuliaji huyo alimuandikia ujumbe wa simu baba yake akisema "Nimevuruga.Nimemiga risasi askari polisi."

Kesi yakabibidhiwa waendesha mashtaka dhidi ya ugaidi

Frankreich Flughafen Paris Orly | evakuierte Passagiere
Uwanja wa ndege wa Orly mjini Paris.Picha: Reuters/B. Tessier

Rais Francois Hollande amesema kesi hiyo imekadhibiwa waendesha mashtaka wa kupambana na ugaidi na kwamba operesheni kadhaa zinaendelea.Amesema kisa hicho kimeonyesha haja ya operesheni ya "Sentinelle" ambayo ilianzishwa kufuatia kuzuka kwa mashabulizi ya wanamgambo hapo mwaka 2015.

Zaidi ya watu 230 wamekufa nchini Ufaransa katika mikono ya washambuliaji wenye mafungamano na kundi la wanamgambo la Dola la Kiislamu ambao ngome zao nchini Syria na Iraq zimekuwa zikishambuliwa na muungano wa kimataifa wenye kuijumuisha Ufaransa.

Mashambulizi ya mabomu yalioratibiwa na mashambulizi ya risasi ni pamoja na yaliotokea mjini Paris hapo mwezi wa Novemba mwaka 2015 mjini Paris ambapo watu 130 waliuwawa na wengine wengi kujeruhiwa.

Kuimarisha usalama kitovu cha kampeni

Frankreich Innenminister Bruno le Roux am Pariser Flughafen Orly
Waziri wa mambo ya ndani wa Ufaransa Bruno le Roux akizungumza na wandishi wa habati katika uwanja wa ndege wa Orly.Picha: picture-alliance/AP Photo/K. Zihnioglu

Kuimarisha usalama wa Ufaransa ni kitovu cha kampeni hiyo ya uchaguzi uliopangwa kufanyika mwezi wa April na Mei ambapo mwanasiasa wa sera za wastani Emmanuel Macron anatabiriwa kutowa upinzani mkali kwa mwanasiasa wa sera kali za mrengo wa kulia Marine Le Pen ambaye anapigia debe kuchukuwa hatua kali dhidi ya wahamiaji walioko nchini humo kinyume na sheria na Waislamu wa itikadi kali.

Walioshuhudia tukio hilo la uwanja wa ndege baada ya kuangushana chini na askari huyo wa kike askari wenzake walijaribu kuzungumza naye bila ya mafanikio ambapo alikimbilia kuteremka ngazi na ndipo alipopigwa risasi.

Mashambulizi hayo ya Jumamosi hayakuwa na taathira kwa ziara ya Mwana mfalme William wa Uingereza ambaye yuko nafasi ya pili katika urithi wa ufalme wa nchi hiyo na mkewe Kate ambao walikuwa wakitarajiwa kukamilisha ziara yao Jumamosi.

Takriban abiria 3,000 waliondolewa katika uwanja wa ndege wa Orly ambao ni wa pili kwa kuwa na harakati kubwa nchini Ufaransa kufuatia kisa hicho ambapo wana usalama walifunga ukumbi wa mapokezi wa uwanja huo na kupekuwa mabomu lakini hakuna vilipuzi viliopatikana.Umma wa abiria ulikuwa nje ukisubiri.

Mwandishi : Mohamed Dahman/ Reuters/AP/

Mhariri :Lilian Mtono