1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BAGHDAD: Mashambulizi ya kujitolea muhanga yaendelea Iraq

26 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBoM

Hadi watu 40 wameua na zaidi ya 150 wamejeruhiwa katika mashambulizi matatu ya kujitolea muhanga, nchini Iraq.Katika mji wa Beiji,kiasi ya kilomita 250 kaskazini ya mji mkuu Baghdad,si chini ya watu 27 waliuawa na wengi wengine walijeruhiwa baada ya mshambuliaji aliejitolea muhanga kujiripua ndani ya lori kwenye kituo cha polisi.

Shambulio jingine lilifanywa kwenye ukumbi wa hoteli mjini Baghdad na limeua hadi watu 13; miongoni mwao walikuwemo wajumbe kadhaa wa Kisunni wa ngazi ya juu kutoka wilaya ya Anbar. Dakika 45 baadae,mshambuliaji mwengine alijiripua ndani ya gari kwenye kituo cha ukaguzi cha majeshi ya Marekani na Iraq,katikati ya mji wa Saniyeh.Wanajeshi 2 wa Kiiraqi waliuawa na 3 walijeruhiwa katika shambulizi hilo.

Waziri Mkuu wa Iraq,Nuri al-Maliki na Rais George W.Bush wa Marekani wamelaani mauaji hayo.Bush alipozungumza mjini Washington alisema,hiyo ni sababu zaidi ya kusaidia juhudi za kidemokrasia na upatanisho nchini Iraq.