1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Abdelaziz Bouteflika bado anashikilia wadhifa wake

Angela Mdungu
28 Machi 2019

Baraza la Taifa la Katiba nchini Algeria bado halijakutana kuamua iwapo Rais Abdelaziz Bouteflika anafaa kubaki madarakani ama la baada jeshi la nchi hiyo kutaka aondolewe, na washirika wake kumtupa mkono.

https://p.dw.com/p/3Fq3z
BdTD - Algerien Polizisten in Algier versuchen Protestierende aufzuhalten
Picha: Reuters/Z. Bensemra

Redio ya taifa ya Algeria imesema, baraza la Taifa la Katiba nchini humo bado halijafanya mkutano wowote hadi sasa kuamua iwapo Rais Abdelaziz Bouteflika anafaa kubaki madarakani ama la baada ya jeshi la nchi hiyo chini ya Jenerali Ahmed Gaed Salah kutaka aondolewe, na washirika wake kumtupa mkono.

Mkuu wa majeshi wa Algeria Luteni Jenerali Ahmed Gaed Salah siku ya jumanne alilitaka baraza la katiba la nchi hiyo, kutumia kifungu cha 102 cha katiba kinacholipa mamlaka baraza la katiba la nchi hiyo kuamua iwapo Rais anao uwezo wa kuendelea kuongoza.

Luteni Salah anatajwa kuwa mfuasi mwaminifu wa Rais Bouteflika ambaye alimfanya kuwa mmoja wa watu wenye nguvu za kisiasa nchini humo amezungumzia hali ya kisiasa ilivyo nchini humo na Kksema kuwa, Algeria iko katikati ya eneo lenye hali tete lisilo na uthabiti na kwamba jeshi lake limekubaliana kupambana dhidi ya vitisho vya aina yoyote, vikiwemo ugaidi, na makundi ya wahalifu ambayo yanawakilisha changamoto kubwa ilizonazo nchi hiyo.

Algerien Abdelaziz Bouteflika und Ahmed Gaid Salah
Rais Bouteflika na Jenerali Ahmed Gaed Salah katika picha ya pamoja ya mwaka 2012Picha: picture-alliance/abaca/K. Mohamed

Jenerali Salah ametoa kauli hiyo katika ngome ya jeshi iliyo Kusini mwa Algeria ,na kauli yake imebeba uzito mkubwa kutokana na ufuasi wake kwa Bouteflika. Aliteuliwa  mnamo mwaka 2004 na Rais Bouteflika kushika wadhfa wa mkuu wa utumishi wa umma wakati alipokuwa akikaribia kustaafu. Uhusiano wa Salah na Bouteflika uliongezeka kutokana na uhuru aliopewa katika kulifanyia jeshi mabadiliko na kulifanya kuwa la kisasa zaidi. Mwezi Julai 2013, Rais alimwongezea madaraka kwa kumpa jukumu la kuwa waziri wa ulinzi. Katika miezi ya hivi karibuni, amekuwa akiunga mkono waziwazi mipango ya Bouteflika ya kutaka kugombea tena urais kwa mhula mwingine.

Uamuzi wa kutangaza iwapo Rais Bouteflika kwa hali yake hawezi kuendelea na wadhifa wake utatakiwa kupitishwa na mbili ya tatu ya walio wengi kwenye Bunge la Algeria. Hiyo itamaanisha kwamba, mwenyekiti wa Bunge Abdelkader Bensalah atakuwa Rais wa muda kwa walau siku 45 baada ya Bouteflika kuondoka madarakani. Wakati hayo yakiendelea, Mamia ya waandamanaji wameendelea kuingia mtaani kumtaka Rais Bouteflika ajiuzulu. Waandamanaji hao wamekaririwa wakipiga kelele kuwa Rais Bouteflika ni mwizi na ameiharibu nchi.

Mwandishi: Angela Mdungu/APE/RTRE

Mhariri: Daniel Gakuba