1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BASRA : Raia wa magharibi waliotekwa waendelea kutafutwa

18 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCrY

Vikosi vya usalama leo vimekuwa vikiendelea kuwatafuta raia wawili wa mataifa ya magharibi waliotekwa nyara kusini mwa Iraq baada ya kurepotiwa kwamba mateka mmoja wa Marekani ameuwawa lakini wengine wawili wameokolewa katika nchi hiyo iliokumbwa na umwagaji damu ambayo Waziri Mkuu wa Uingereza Tony Blair amekiri kuwa hali ni ya maafa.

Raia hao watano wa mataifa ya magharibi wanne wakiwa ni raia wa Marekani na mmoja wa Austria wanaofanya kazi kama walinzi wa usalama wa kampuni moja ya Kuwait walitekwa nyara hapo Alhamisi wakati wakisindikiza msafara wa magari makubwa ya mizigo 49 karibu na mji wa kusini wa Safwan.

Utekaji nyara huo umetokea ikiwa ni siku mbili tu baada ya kutekwa nyara kwa madarzeni ya watu kutoka jengo la wizara ya serikali mjini Baghdad ambao wengi wao hadi hivi sasa hawajulikani walipo.

Wakati huo huo Uingereza inapanga kuongeza msaada wake kwa Iraq kwa euro milioni 150 katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Waziri wa Fedha wa Uingereza Gordon Brown ametangaza hayo wakati wa ziara yake katika mji huo wa kusini wa Iraq Basra. Brown anatajwa sana kuchukua nafasi ya Waziri Mkuu wa Uingereza Tony Blair wakati atapon’gatuka hapo mwakani.