1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern haina mshindani katika Bundesliga

Sekione Kitojo
15 Januari 2018

Bayern Munich wanaelekea  kulinyakua  tena  taji  la  Bundesliga msimu  huu baada  ya  mwishoni  mwa  juma  kufikisha  mwanya wa pointi  13 kutoka  timu  inayoifuatia.

https://p.dw.com/p/2qsSI
Fußball Bundesliga Bayer Leverkusen - Bayern München 2018
Wachezaji wa Bayern Munich Frank Ribbery na Rafinha wakishangiria baoPicha: Reuters/W. Rattay

 

Tuanze  na  Bundesliga: Borussia  Dortmund  ilitoka  sare  ya  bila kufungana  jana  Jumapili  na  VFL Wolsburg,  ambao  ni  vidume  wa kutoka  sare  katika  Bundesliga. Borussia  Dortmund  iliteremka dimbani  jana  bila  jogoo  wake mshambuliaji  nyota  Pierre-Emerick Aubameyang , ambaye  aliondolewa  katika  kikosi  hicho  kwa  mara nyingine  tena  kwa  kushindwa  kufika  katika  kikao  cha  timu. Kocha  wa  Borussia  Dortmund Peter Stoeger  amezungumzia kuhusu  suala  hilo na  kusema.

FSV Mainz 05 - Borussia Dortmund
Kocha wa Borussia Dortmund Peter StoegerPicha: picture alliance / Thomas Frey/dpa

"Mimi  binafsi  hiyo si  kitu kwa  kweli , ni  lazima  niseme. Tatizo  ni kwamba kwangu  mimi  sielewi, kwa  nini, kwa  kuwa  anafanya mazowezi  vizuri  tu, na  siwezi  kuwaambia  hasa,  kwa  nini anafanya  hivi  mara  nyingi. Nina uvumilivu  vya  kutosha. Najaribu mambo  mengi  kuyaweka  sawa. Lakini  nikijisikia  kwamba , haiwezekani  tena,  nachukua  uamuzi  kama  huo, lakini  binafsi sijisikii  vibaya. Kwanza  kabisa  namthamini  sana  pamoja  na hayo. Lazima atakuwa  na  sababu, nina matumaini  hayo,  na namkubali. Nadhani  hana  matatizo.

Aubameyang  ambaye  alikuwa  mfungaji  bora  wa  ligi  msimu uliopita, anatoa  changamoto  kwa  uvumilivu  wa  Borussia Dortmund. Aliondolewa  kutoka  katika  kikosi  cha  timu  hiyo  katika mchezo  wa  jana  dhidi  ya  Wolfsburg  kwa  kukosa  mkutano  wa timu,  na  hatua  ya  Aubameyang  kukiuka  nidhamu  kunafuatia kuondolewa  pia  katika  kikosi  mwezi Novemba  kwa  kupiga  picha ya  video  ambayo  hajaruhusiwa  katika  uwanja  wa  mazowezi  wa klabu  hiyo.

1. Bundesliga 15. Spieltag | Borussia Dortmund - Werder Bremen | Pierre-Emerick Aubameyang
Mshambuliaji Pierre-Emerick Aubameyang wa Borussia DortmundPicha: Reuters/T. Schmuelgen

Pia  aliondolewa  kutoka  katika  kikosi  hicho  msimu uliopita kwa  kusafiri  kwenda  Milan  Italia  muda  mfupi  kabla  ya mchezo  wa  Champions League. Aubameyang  mwenye  umri  wa miaka  28  amefumania  nyavu  mara  13  msimu  huu  katika michezo  15  ya  ligi , huku  kukiwa  na  ripoti  za  kutakiwa   na  klabu nchini  China  na  pia  Arsenal London.

Iwapo hataki  kucheza  hapa , tutampa  nafasi  yake  mtu mwingine,"  amesema  kocha  wa  Dortmund Peter Stoeger.  Kuhusu mchezo  wa  jana  dhidi  ya  Wolfsburg  na  kupoteza  nafasi  nyingi za  wazi  za  kupata  bao mlinda  mlango  wa  Borussia  Dortmund Roman Burki  alisema.

"Ukiangalia  mchezo  wenyewe, nadhani , kila  upande ulipata  nafasi za  kufunga. Nafikiri  pia , tungeweza  kupata nafasi nyingi  zaidi , iwapo  tungecheza  vizuri  zaidi  na  kushambulia  hadi  mwisho. Hilo tulipaswa  kulifanya  vizuri  zaidi. Inasikitisha  kwetu  kwamba tumeambulia  pointi moja  tu."

Bundesliga yarejea uwanjani

Katika  ufunguzi  wa  dimba  la  Bundesliga  siku  ya  Ijumaa, Bayern Munich  ilifanikiwa  kutoa  ishara  kwa  timu  zote  za  Bundesliga kwamba  mara  hii  tena  wako  njiani  kulipeleka  taji  la  Bundesliga mjini  Munich  na  hali  hiyo  haitabadilika. Bayern  Munich wakikaribishwa  nyumbani  na  Bayer Leverkusen  waliuteka  uwanja wa  Bay Arena  kwa  kuizaba  Bayer Leverkusen  bila  taabu  kwa mabao 3-1  kama  ilivyokuwa  katika  mchezo  wa  kuanza  ligi  ya msimu  huu 2017 /18.

Fußball Bundesliga Bayer Leverkusen - Bayern München 2018
Julian Brandt(kushoto) wa Leverkusen na Arjen Robben wa Bayern wakipambana Picha: Reuters/W. Rattay

Timu  iliyotoka  uwanjani  na  kicheko  na  kifua  mbele  zaidi  wiki  hii hata  hivyo  ilikuwa  FC Kolon  ambayo  ilifanikiwa  kwa  mara  ya pili  msimu  huu  kupata  pointi  zote 3  baada  ya  kuwangusha Borussia  Moenchengladbach  kwa  mabao 2-1  kwa  bao  safi  la dakika  za  majeruhi  la  Simon Terodde  aliyerejea  hivi  karibuni kutoka  Wolfsburg  alikoanzimwa.

FC Kolon  imekusanya  sasa pointi  9  ikiwa  bado  inashiklilia  mkia  lakini  ushindi  wa  jana ni dalili  ya  kufufuka  na  kupambana  kujiondoa  kutoka  katika  hatari ya  kushuka  daraja. Huyu  hapa  mfungaji  wa  bao  hilo  muhimu  la ushindi  kwa  FC Kolon Simon Terodde.

1. FC Koeln v Borussia Moenchengladbach - Bundesliga
Wachezaji wa FC Kolon wakimpongeza mwenzao Terodde (namba 4) baada ya kufunga bao dakika za mwisho za mchezoPicha: Getty Images/L. Baron

"Sina  maneno  ya  kuelezea, Katika  dakika  za  mwisho  nilikuwa bila  kujijua  nilikimbilia  karibu ya  nguzo ya  goli. ilikuwa  ni  krosi nzuri  sana , nilipeleka  mwili  wangu kuelekea  mpira, na  kuupeleka katika  nyavu ndogo, safi  sana. Baada  ya  hapo sikukumbuka  kitu tena chochote kilichotokea. Nafikiri , kulikuwa  na  watu  kumi  ama kumi  na  tano  wako  juu  yangu. Ulikuwa  ushindi  muhimu  sana leo."

Mario Gomez

Mchezaji  wa  kiungo  wa  Borussia  Moenchengladbach  Patrick Herrmann  alikuwa  na  haya  ya  kusema  kuhusiana  na  kipigo hicho.

"Haieleweki  kabisa. Ni  mchezo  wenye  machungu sana , hatujawahi  kushindwa  namna  hii. Hasa  katika  mchezo  wa  Derby katika  dakika  za  mwisho  tunafungwa  bao  na  Kolon,  inaumiza sana. na  katika  kipindi  cha  pili  tulikuwa  timu  bora  kabisa uwanjani , tulipata  nafasi  mbili, nzuri  za  kufunga  na  tulipaswa kushinda  mchezo  ule."

Stuttgart  nayo  ikimkaribisha  kijana  wao  aliyerejea  nyumbani Mario Gomez  ilifanikiwa  kupata  ushindi  wa  bao 1-0  nyumbani dhidi  ya  Hertha  Berlin , kwa  goli  ambalo  mlinzi  wa  Hertha  Berlin Niklas Stack  alijifunga  mwenyewe.

Fußball Bundesliga VfB Stuttgart - Hertha BSC
Mshambuliaji wa Stuttgart Mario Gomez(kushoto) akipambana na mlinzi wa Hertha Berlin Niklas StarkPicha: picture-alliance/dpa/M. Murat

Hannover  ikairarua  Mainz 05  kwa  mabao 3-2.

RB Leipzig  inashikilia  hivi  sasa  nafasi  ya  pili  katika  msimamo wa  ligi  kwa  kuwa  na  pointi 31 wakifuatiwa  na  Schalke  04  yenye pointi 30 na Borussia  Dortmund  iko  katika  nafasi  ya  4 ikiwa  na pointi 29 , wakati  Bayer Leverkusen na  Borussia Moenchengladbach  zinashikilia  nafasi  ya  kucheza  katika  Europa League  kwa  sasa  katika  nafasi  ya 5  na  6.

Fußball Bundesliga RB Leipzig - FC Schalke 04
Mchezaji wa kati wa RB Leipzig Naby KeitaPicha: Getty Images/AFP/R. Michael

Werder Bremen  kwa  kutoka  sare  na  Hoffenheim  siku  ya Jumamosi  haikusogea  mbali  sana  na  eneo  la  hatari  ya  kushuka daraja , na  iko  nafasi  ya 16, Hamburg SV  ambayo  miaka  minne iliyopita  imeendelea  kusumbuka  kujinasua  kutoka  kushuka  daraja bado  iko  katika  hatari  hiyo  msimu  huu  ikiwa  na  pointi 15  na katika  nafasi  ya  17.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo  / afpe / rtre / ape /

Mhariri: Yusuf , Saumu