1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern, Hertha zaongeza kasi katika Bundesliga

Bruce Amani
24 Septemba 2018

Bundesliga imechukua taswira ya kawaida ikiwa ni mechi nne tu baada ya msimu kuanza. Bayern Munich wanaongoza kileleni, lakini Hertha Berlin ndio wanashikilia nafasi ya pili

https://p.dw.com/p/35PEV
Bundesliga 4. Spieltag | FC Schalke 04 vs. Bayern München | Elfmeter Lewandowski
Picha: Reuters/L. Kuegeler

Berlin wako nyuma ya Bayern na pengo la pointi mbili  na sasa watacheza ugenini katika mechi muhimu dhidi ya nambari nne Werder Bremen kesho Jumanne kabla ya kuwaalika Bayern Ijumaa katika mechi ambazo sasa huenda zikaamua namna watakavyofanya msimu huu.

Hertha iliibamiza Borussia Moenchengladbach 4-2 mwishoni mwa wiki. Bayern nao watakuwa nyumbani dhidi ya majirani Augsburg.

Kichapo cha Schalke dhidi ya Bayern kiliwaacha mkiani mwa ligi na kuwa timu pekee ambayo haijapata pointi yoyote mpaka sasa. Watajaribu kuifufua kampeni yao kwa kupambana na Freiburg. Hanover na Hoffenheim itakamilisha mechi za kesho wakati Jumatano, Borussia Dortmund, timu nyingine ambayo haijapoteza mchezo mpaka sasa kwenye ligi, itawaalika wageni Nuremberg.

BVB wako katika nafasi ya tatu kwa sasa, na tofauti ya mabao mbele ya Bremen, baada ya kupata pointi moja katika sare yao ya 1-1 na Hoffenheim Jumamosi. Nuremberg wako nafasi ya nane huku wageni wengine kwenye ligi Fortuna Dusseldorf wakiwa nafasi ya tisa, kabla ya kuwaalika Bayer Leverkusen.

RB Leipzig watawaalika VfB Stuttgart na Gladbach itajaribu kujinyanyua dhidi ya Eintracht Frankfurt. Mechi ya mwisho itakuwa mpambano kati ya nambari saba Mainz dhidi ya nambari tano Wolfsburg, ambao walipewa kichapo cha kwanza msimu huu dhidi ya Freiburg mwishoni mwa wiki.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman