1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich yafuta aibu ya Barcelona

13 Aprili 2009

Wolfsburg yaongoza bado bundesliga.Munich yailaza Frankfurt.

https://p.dw.com/p/HVpM
Wolfsburg inaendelea kutamba.Picha: AP

Katika Bundesliga,mabingwa Bayern Munich wamefuta kidogo ile aibu waliopakwa na FC Barcelona kwa ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Frankfurt -Hamburg ilikosa jana nafasi ya kuibuka pointi sawa na viongozi wa Ligi Wolfsburg kwa kukomewa bao 1:0 na Stuttgart.Frederico Macheda aliwika tena kwa Manchester United na sasa Manu imeipokonya Liverpool usukani wa kuongoza Ligi ya Uingereza.

Wolfsburg ilitoka nyuma Jumamosi na kuzima vishindo vya Borussia Moenchengladbach na kuondoka na pointi 3 ilizohitaji kubakia kileleni mwa Bundesliga:Mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich walfedheheshwa kwa mabao 4-0 mjini Barcelona kati ya wiki iliopita. Munich ikijua hatima ya kocha wao Jurgen Klinsman iko mashakani, walicheza kumuokoa na kuokoa pia heshima ya Bayern munich.Alikuwa mfaransa Franck Riberry alielifumania kwanza lango la Frankfurt kwa m kwaju mkali na maridadi ulionasa wavuni tayari katika kipindi cha kwanza.Baadae mshambulizi Luca Toni,akatia bao la pili.Hata mlinzi wa Brazil,Lucio alitikisa wavu wa Frankfut na mwishoe , ikawa zamu ya Bastian Schweinsteiger kutia bao la 4.Frankfurt haikuwa na jibu kwa hujuma za Munich siku hiyo.

Kocha wa Bayern Munich,Jurgen Klinsmann ,alivuta pumzi kwani kashfa ya mjini Barcelona kwa mabingwa wa Ujerumani wiki iliopita, ilikuwa kubwa.Binafsi alisema:

"Jinsi timu yetu ilivyojibisha msukosuko wa aibu tuliopata Barcelona,imefurahisha sana.

Mapigo tuliopata yatupasa kwanza kuponesha majaraha.Sote-kocha,wachezaji,viongozi ilitupasa kwanza tumeze shubiri,kwani yaliotokea Barcelona yalituuma sana."Wolfsburg iliotamba kwa mabao 2-1 mbele ya Borussia Moenchengladbach sasa wanaongoza Bundesliga kwa pointi 3 mbele ya Bayern Munich,mabingwa. Hamburg wana pointi 51 na laiti wangelishinda jana walipocheza na Stuttgart, basi wangekuwas hirimu sawa na Wolfsburg.Hertha Berlin, ambayo wakati mmoja iliongoza Ligi hii, imo kurudi nyuma: Kwani, ilichapwa mabao 2:0 na Hannover na imeangukia sasa nafasi ya 4 ya ngazi ya Ligi.

Berlin itacheza mpambano ujao bila jogoo lao Andrey Veronin,kwani muukrain huyo alioneshwa kadi nyekundu na kutolewa nje ya uwanja kwa kufanya madhambi uwanjani.,Berlin itatembelewa na bremen mwishoni mwa wiki ijayo.Schalke ,imepiga hatua kukaribia tikiti ya kucheza Kombe la Ulaya la UEFA kufuatia ushindi wo wa mabao 2-0 dhidi ya Karlsruhe,inayoburura mkia.Kevin Kuranyi, aliwapatia bao la kwanza mnamo dakika ya 24 ya mchezo kabla Jefferson Farfan kutia bao lao la pili.

Katika changamoto ya mkiani wa Ligi,Cottbus ilijiokoa kwa pointi 3 kwa kuitandika Armenia Bielefeld. Chipukizi Hoffenheim walioanza msimu kwa vishindo wanaendelea kupungua kasi.Kwani, wamezabwa mabao 3-0 na Bochum tena nyumbani mwao.Borussia Dortmund iliiambia FC Cologne kutangulia si kufika.Ilifuta bao la Cologne la kipindi cha kwanza na halafu kuwakomea mabao 2 mengine na kuondoka na ushindi wa manao 3:1.

Katika Premier League-Ligi ya Uingereza, FEDERICO MACHEDA amewika tena kwa bao lake lililoifanya Manchester united kurudi kileleni mwa premier League.Liverpool ilishika usukani jumamosi ilipoikomea Blackburn Rovers mabao 4-0.Lakini, Manu ikitamba wakati huu na Macheda ,ilitoa jibu dakika za mwisho za changamoto na Sunderland na kuondoka na ushindi wa mabao 2-1.Chelsea ilivuka salama katika zahama za Bolton Wanderes na mwishoe ilitamba kwa mabao 4-3 .Chelsea sasa iko nafasi ya 3 au pointi 3 nyuma ya Liverpool.Manchester United ingali ina mpambano mmoja wa kucheza.

Muandishi: Ramadhan Ali

Mhariri: M.Abdulrahman