1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BBI yapitishwa na zaidi ya kaunti 24

Shisia Wasilwa
23 Februari 2021

Taifa la Kenya linaelekea kwenye kura ya maoni baada ya zaidi ya kaunti 24 kuidhinisha muswada wa marekebisho ya katiba ya mwaka 2020.

https://p.dw.com/p/3pl3x
Kenia Building Bridges Initiative (BBI)
Picha: AFP/T. Karumba

Kufikia Jumanne jioni ni kaunti 30 zilizokuwa zimeuidhinisha. Muswada huo sasa utawasilishwa katika bunge la taifa na baraza la seneti kabla ya kuidhinishwa na rais.

Hatua hiyo inajiri licha ya onyo kutoka kwa baadhi ya viongozi wa Mlima Kenya kuwa Mpango wa Maridhiano ulikosa umaarufu katika kaunti tisa kati ya kumi zinazopatikana katika eneo hilo.

Soma zaidi:Kenya kuwanunulia wawakili wa kaunti magari ya dola mil.41

Eneo linalofahamika kuwa ngome ya kisiasa ya Rais Uhuru Kenyatta. Kupitishwa kwa muswada huo na mabunge 30 ni pigo kwa Makamu wa Rais William Ruto ambaye amekuwa akiupinga muswada huo kama unaolenga kubuni nafasi za kazi kwa viongozi.

Mabunge mawili ambayo yana wabunge na maseneta wengi wanaomuunga mkono Rais Kenyatta na kiongozi wa chama cha upinzani cha ODM, Raila Odinga yanatarajiwa kuupitisha kabla ya wananchi kuupigia kura.

William Ruto amekuwa akiipinga BBI

Kenia Amtseinführung Präsident Kenyatta
Naibu Rais William RutoPicha: picture-alliance/abaca/Kenyan Presidency Press Office

Ruto amekuwa akizunguka nchi nzima akidai kuwa muswada huo unalenga kuwapa uongozi matajiri badala ya walalahoi ambao wamekuwa wakitengwa.

Muswada huo unaopendekeza kupanuliwa kwa uongozi wa serikali kuu kwa kuongeza wadhifa wa waziri mkuu na manaibu wake wawili uliundwa machi mwaka 2018 baada ya salamu za heri kati ya Rais Kenyatta na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga baada ya matokeo ya uchaguzi wa urais yaliyozua utata mwaka 2017.

Waasisi wake wanalenga kuzima ghasia za kila baada ya uchaguzi mkuu kwa kuyajumuisha makabila mengine. Raila amejitokeza kuwa mtetezi mkuu wa mpango huo licha ya upinzani.

Hata hivyo, wataalam wa masuala ya siasa wanasema kuwa, muswada huo umepata uungwaji mkono katika mabunge ya kaunti baada ya Rais Kenyatta kuwaahidi kuwapa ruzuku ya magari yenye kiasi cha shilingi milioni mbili za Kenya.

Baadhi ya kaunti za Mlima Kenya zilizoupitisha muswada huo ni pamoja na Laikipia, Nyeri, Murang'a, Nyandarua, Tharaka Nithi, Nakuru, Kirinyaga na Meru.

Hatua ya kupitishwa kwa muswada huo katika mabunge ya kaunti ni ushindi kwa Rais Kenyatta na Odinga, ambao wanakusudia kutoa mwelekeo wa siasa za taifa, litakapokuwa likishiriki kwenye uchaguzi mkuu mwakani.