1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BERLIN : Amri kuwauwa waliotaka kuasi

13 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBZs

Nchini Ujerumani waraka uliotangazwa mwishoni mwa juma umetowa ushahidi mpya wa amri zilizoandikwa kwa maandishi kuwataka wanajeshi wa iliokuwa Ujerumani ya Mashariki kuwauwa kwa kupiga risasi watu wanaotaka kuasi wakiwemo wanawake na watoto kwa kukimbilia Ujerumani magharibi.

Waraka huo wa tarehe Mosi mwezi wa Oktoba mwaka 1971 uliogunduliwa wiki iliopita kwenye ofisi ya kuhifadhi nyaraka ya mkoa katika mji wa mashariki wa Magdeburg unaonyesha kwamba Wizara ya Nchi kwa ajili ya usalama ya Ujerumani ya Mashariki iliokuwa ikijulikana kwa jina la Stasi iliwaambia walinzi kwamba lazima wawazuie au kuwauwa wapinzani.

Hubertus Knabe mkuu wa Kumbukumbu ya Wahanga wa Stasi mjini Berlin anasema hapa mtu kwanza kabisa ana ushahidi wa maandishi wa amri ya kuuwa.Huo ni uchochezi wa mauaji au ni uchochezi wa mauaji yasio ya kukusudia na maoni yake ni kwamba waendesha mashtaka wa serikali katika mji wa Magdeburg hivi sasa wanatakiwa wayakinishe iwapo kumefanyika tendo la uhalifu.

Naye Mariannne Birthler ambaye anaongoza mamlaka ya kutunza nyaraka ya polisi wa siri wa Stasi wa Ujerumani Mashariki amesema waraka huo ni muhimu kwa sababu viongozi wa kisiasa wa wakati huo wanaendelea kukanusha kwamba kulikuwepo amri za kuwauwa watu kwa kuwapiga risasi.