1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden: Watu zaidi huenda wakafa Trump asipotoa ushirikiano

Amina Mjahid
17 Novemba 2020

Hatua ya Donald Trump kukataa kushindwa katika uchaguzi wa Novemba 3 nchini Marekani, inaleta ugumu kwa timu ya rais mteule Joe Biden kuratibu masuala muhimu ikiwemo mipango ya kusambaza chanjo ya ugonjwa wa COVID 19

https://p.dw.com/p/3lOYk
USA | Joe Biden designierter Präsident | Rede in Wilmington
Picha: Andrew Harnik/AP Photo/picture alliance

Biden amesema Donald Trump kukataa kukubali kuwa alishindwa katika uchaguzi wa urais na kushindwa pia kupanga hatua za kukabidhi madaraka, huenda kukasababisha watu wengi zaidi kufariki kutokana na ugonjwa wa COVID 19.

Utawala wa Trump haujamkubali Rasmi Biden kama rais mteule, hii ikimaanisha kwamba Biden na timu yake hawawezi kufikia ripoti za kijasusi zinazotolewa juu ya masuala ya usalama wa kitaifa na pia hawawezi kuja na mipango ya kusambaza chanjo ya maradhi ya ugonjwa huo.

"Watu wengi huenda wakafariki iwapo hatutashirikiana," alisema Biden katika mkutano na waandishi habari mjini Wilmington katika jimbo lake la Delaware.

Bidenameongeza kuwa iwapo watasubiri hadi Januari 20 kuanza mipango ya kuendesha nchi, watakuwa wamerejea nyuma kwa mwezi mmoja, kwa hiyo nilazima na muhimu kwa shughuli kuanza sasa.

Washington Präsident Trump | PK Impfstrategie
Rais Trump amekataa kukubali kushindwa katika uraisPicha: MANDEL NGAN/AFP

Kulingana na rais huyo mteule wa Marekani huku wakipambana na ugonjwa wa COVID ni lazima wahakikishe kuwa biashara na wafanyakazi wana vifaa vya kutosha, rasilimali, muongozo wa kitaifa na kiafya na kuwa katika viwango vizuri vya usalama ili kufanya kazi kwa usalama mzuri zaidi. Hata hivyo katika suala la Trump kukataa kushindwa katika uchaguzi uliopita Biden alisema analiona suala hilo kuwa la aibu kwa Marekani.Trump alitaka kuishambulia Iran wiki chache kabla kuondoka madarakani

Biden na Makamu wake wa rais Kamala Harris wameendelea kufanya mikutano ya mwanzo na viongozi wa miungano ya wafanyakazi na wakuu wa makampuni makubwa ikiwemo General Motors na Gap Inc. Katika mazungumzo hayo, Biden amesema pande zote zimekubaliana kuwa mikakati ya kitaifa inapaswa kuchukuliwa kusaidia kudhibiti kusambaa zaidi kwa virusi vya corona na kwamba kuna kazi kubwa ya kufanywa kuziba mapengo yaliopo katika uchumi wa Marekani ulioyumba kutokana na janga hilo.

Biden pia ameliomba bunge kupitisha mfuko wa dharura utakaowasaidia wafanyabiashara na wafanyakazi walioathirika na janga la corona na kupiga jeki pia maendeleo zaidi ya chanjo ya ugonjwa huo. Joe Biden amesema kwa sasa Marekani inaelekea katika kipindi cha kiza cha msimu wa baridi mambo huenda yakawa mabaya zaidi kabla ya kunyooka tena.

Marekani ina watu zaidi ya milioni 11.2 wanaugua ugonjwa wa COVID 19 idadi ambayo ni kubwa duniani.