1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bolton aiambia Iran 'busara' sio 'udhaifu'

Bruce Amani
23 Juni 2019

Mshauri wa Usalama wa Taifa nchini Marekani John Bolton amesema kuwa Iran haipaswi "kukosea kuichukulia hatua za busara za Marekani kuwa udhaifu,”

https://p.dw.com/p/3KwgL
US-Präsident Trump mit Sicherheitsberater John Bolton
Picha: Getty Images/C. Somodevilla

Ujumbe mkali wa Bolton ulionekana kuilenga sio tu Iran, bali pia kuwahakikishia washirika wa Marekani kuwa Ikulu ya White House inadhamiria kuongeza shinikizo dhidi ya Iran. Israel, pamoja nan chi za Ghuba ya Uarabuni zinaichukulia Iran kuwa kitisho chao kikubwa na hatua ya dakika ya mwisho ya Trump kusitisha shambululizi inaonekana kuibua maswali kuhusu nia ya Marekani kutumia nguvu dhidi ya Jamhuri hiyo ya Kiislamu.

Kuangushwa kwa ndege hiyo ya Marekani isiyoruka na rubani imeufikisha mzozo wao katika kiwnango kingine cha juu katika Ghuba ya Uajemi.

Utawala wa Trump umeapa kujumuisha kampeni yenye shinikizo kubwa ya vikwazo vya kiuchumi na kupeleka wanajeshi wake katika kanda hiyo, baada ya Marekani kujiondoa katika mkataba wa nyuklia wa Iran na mataifa yenye nguvu duniani mwaka wa 2015.

US-Drohne Global Hawk
Ndege ya Marekani isiyoruka na rubani Picha: picture-alliance/US Air Force/Zumapress

Akizungumza mjini Jerusalem pamoja na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ambaye naye ni mkosoaji mkubwa wa Iran, Bolton amesema hakuna aliyewapa leseni ya uwindaji katika Mashariki ya Kati. Ameongeza kuwa rais Trump alisema kuwa "alisitisha tu shambulizi alilokuwa amepanga dhidi ya Iran kwa wakati huu..”

Iran imesema leo kuwa haitojobu kitisho chochote dhidi yake na kuonya kuhusu hatari iliyopo kama kutakuwa na makabiliano ya kijeshi. Meja Jenerali Gholamali Rashid amesema kama mgogoro utazuka katika kanda hiyo, hakuna nchi itakayoweza kuhimili athari zake.

Bolton anafanya ziara nchini Iran kwa ajili ya mazungumzo ya pande tatu na wenzake wa Israel na Urusi ambayo yanatarajiwa kuangazia kujihusisha kwa Iran katika mizozo ya kanda hiyo, ikiwemo katika nchi jirani Syria.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameonya leo kuwa ni muhimu kuepusha aina yoyote ya mabishano katika eneo la Ghuba. Amesema ulimwengu kwa sasa hauhitaji mgogoro mkubwa katika Ghuba.