1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Borussia Dortmund yakosa mwelekeo

Sekione Kitojo
30 Oktoba 2017

Borussia Dortmund imetumbukia katika mzozo baad ya kushindwa kupata matokeo mazuri mnamo wiki tatu, yapoteza uongozi wa ligi  dhidi ya Bayern Munich, na yakaribia pia kuaga michuano ya Champions League.

https://p.dw.com/p/2mkzW
Deutschland Hannover 96 - Borussia Dortmund
Wachezaji wa Borussia Dortmund Mario Götze (kushoto) na Nuri Sahin (kulia)Picha: picture alliance/dpa/P. Steffen

Tukianza  na  Bundesliga, Borussia  Dortmund imetumbukia  katika hali  ya  sintofahamu  baada  ya  kushindwa  kupata  matokeo mazuri katika  michezo  mitatu ya  ligi  ambapo  imeambulia  pointi moja tu  na  kufungwa  takriban  mabao 9 na  kuweka  wazi  udhaifu wa  safu  ya  ulinzi  ya  timu  hiyo. borussia  Dortmund imeshindwa mwishoni  mwa  wiki  kutetea  uongozi  wake  wa  ligi  na kukubali kipigo  cha  mbwa  mwizi  baada  ya  kukandikwa  mabao 4-2  na timu  iliyopanda  daraja  msimu  huu Hannover 96  kipigo  kilicholeta gumzo  kubwa  kuhusu  kocha  mkuu  Peter Bosz  kwamba  hana plan B wakati  timu  ikiwa  imekwama  katika mpango  wa  kwanza. Mlinda  mlango  wa  Borussia  Dortmund  anatathmini  kuhusu mchezo  ulivyokuwa.

Deutschland Hannover 96 - Borussia Dortmund
Pambano kati ya Hannover 96 dhidi ya Borussia DortmundPicha: picture alliance/dpa/C. Jaspersen

"Tulijua , kwamba  ni  timu  nzuri.  wanafanyakazi  kama  timu, na  leo wameonesha  hivyo. Wana wachezaji , wawili ama  watatu , ambao wanafanyakazi  vizuri  sana. Hatukuweza  kabisa  kufanya  vizuri upande wa  ulinzi. Tulishindwa  kabisa  mapambano  ya mtu na  mtu. Hii nazungumzia  pamoja  na  mimi  binafsi. Bila shaka utapata kipigo unapokutana na timu nzuri."

Borussia  Bortmund  hivi  sasa  inashika  nafasi  ya  pili nyuma ya mabingwa  watetezi  Bayern Munich. Bayern  hivi  sasa  ina  pointi 23 tatu  zaidi  ya  Borussia  Dortmund  baada  ya  kuiandika  RB Leipzig  kwa  mabao  2-0  katika  mchezo  mwingine uliokuwa  na mivutano  kadhaa  na  maamuzi  ya  kutatanisha. RB Leipzig inabakia  katika  nafasi  ya  tatu  ikiwa  na  pointi 19.

Hannover baada  ya  kuangusha  mbuyu siku  ya  Jumamosi  dhidi  ya Borussia  Dortmund  sasa  imepanda  hadi  nafasi  ya  nne ikiwa  na pointi 18 , FC Schalke 04  imeingia  katika  nafasi  ya  juu  kwa  mara ya  kwanza  katika  kipindi cha misimu  miwili  ikiwa  katika  nafasi ya  tano  baada  ya  kutoka  sare  na  Wolfsburg  kwa  kufungana bao 1-1.

Fußball Bundesliga FC Schalke 04 - VfL Wolfsburg
Mshambuliaji wa Schalke 04 Franco Di santo(kushoto) akipambana na Maximilian Arnold Picha: picture-alliance/dpa/G. Kirchner

FC Kolon  bado inagagaa  katika  nafasi  ya  mkiani  mwa  ligi  ya Ujerumani  baada  ya  kupokea  nayo  kipigo  cha  mabao 2-1  dhidi ya  watani  wao wa  jadi Bayer 04 Leverkusen. Wakati  Leverkusen imesogea  nafasi  moja  kutoka  ya  tisa  hadi  ya  nane  ikiwa  na pointi 15 , FC Kolon imebakia  na  pointi  2  tu  kibindoni.

Kocha Nagelsmann akasirishwa na kipigo

Baada  ya  kipigo  cha  mabao 3-1 dhidi  ya Borussia Moenchengladbach, kocha  wa  Hoffenheim  alikasirishwa  sana  na timu  yake  inavyocheza na  kutupa  chupa  ya  maji  ambayo iliangukia  kwa  mashabiki  na  hatimaye  kutakiwa  na  refa  kwenda kuangalia  kandanda  akiwa  na  mashabiki  badala  ya  benchi la ufundi.

"Nashukuru  Mungu  kwamba  haikumpata  mtu, badala  yake iligonga ukutani. Iliporudi chupa ilimgonga shabiki. Na  ndipo nilipoamriwa kwenda  kukaa jukwaani  na  naomba  radhi kwa  kitendo  hicho. samahani  sana, kutokana  na  kitendo  changu  cha  kijinga, ambacho  hakikupaswa  kutokea na  sitafanya  tena. Nilimkumbatia, na  hata  kama  angekuwa  shabiki  wa  Gladbach ningemkumbatia. Isingekuwa  rahisi  lakini  ningejaribu."

Fußball Bundesliga TSG 1899 Hoffenheim - Borussia Mönchengladbach Julian Nagelsmann
Kocha wa TSG 1899 Hoffenheim Julian NagelsmannPicha: Imago/T. Frey

Werder  Bremen  ilikandikwa  mabao 3-0 na  Augsburg  na  kubakia katika  nafasi  ya  17 ikiwa  na  pointi  5  tu  katika  michezo  10 . Ndio  sababu  leo  hii  timu  hiyo  imetengana  rasmi  na  kocha wake  mkuu Alexander Nouri .  Klabu  hiyo  kutoka  kaskazini  mwa Ujerumani  imethibitisha  leo  Jumatatu   chini  ya  masaa  24  baada ya  kubungizwa  mabao 3-0  na  Augsburg  nyumbani.

Nouri  aliteuliwa msimu  uliopita  na  kuiongoza  klabu  hiyo kuepuka  kushuka  daraja na  kukaribia  kuingia  katika  nafasi  za  kucheza  kombe  la  ligi  ya Ulaya. Lakini  sare tano na  kichapo  mara  tano  vimemgharimu kocha  Nouri  kibarua  chake. Mshambuliaji  wa  Werder  Bremen  na nahodha  wa  timu  hiyo Zlatko Junuzovic anasema.

"Matokeo  ni  mabaya, hali  ni mbaya. Hatuwezi  hivi  sasa kulalamikia hali  hii  au  lolote lile. Tumejiingiza  wenyewe  katika  hali hii. Wenyewe ndio tunamakosa na  lazima  tujitoe. Sijui , ni  vipi  au nini  kinakuja, lakini hatimaye , bila  kujali nini  kimetokea, kama  timu inatubidi kusimama  pamoja  na  kuonesha  uwezo  wetu uwanjani."

Deutschland Bundesliga Alexander Nouri, Trainer SV Werder Bremen
Kocha wa zamani wa Werder Bremen Alexander Nouri ambaye kibarua kiliota majani baada ya mfululizo wa vipigo Picha: picture-alliance/nordphoto/Ewert

Kocha msaidizi

Werder Bremen  imesema  kocha  wake  wa  timu  ya  vijana  wa chini  ya  miaka  23  Florian Kohfeldt , pamoja  na  kocha  msaidizi Thomas Horsch  wa  kikosi  cha  vijana  wa  chini  ya  miaka  17 na kocha  msaidizi  wake  Tim Borowski wataitayarisha  timu  hiyo  kwa ajili  ya  pambano  la  ligi  hapo Ijumaa  ikiifuata  Eintracht  Frankfurt.

Katika  kombe  la  shirikisho  nchini  Ujerumani maarufu  kama  DFB Pokal , hivi  sasa  likiingia  katika  duru  ya  robo  fainali,  Bayern Munich  ambayo  imelinyakua  kombe  hilo  mara  nyingi  zaidi inawasubiri  katika  duru  yaq  timu 16  zilizobakia  Borussia dortmund  mabingwa  watetezi  wa  kombe  hilo.

Timu  hizo  za  juu katika  Bundesliga  kwa  sasa  zimepambana  katika  fainali  mwaka 2012, 2014 na 2016. Katika  misimu  iliyopita  vilabu  hivyo zimekutana  katika  nusu  fainali, na  BVB  ilishinda  mpambano  huo kwa  mabao 3-2  mjini  Munich msimu  uliopita na  hatimaye kunyakua  ubingwa  dhidi  ya  Frankfurt.

Deutschland Bayern München - RB Leipzig | Jubel
wachezaji Robert Lewandowski na Arjen Robben wa bayern MunichPicha: picture alliance/dpa/T. Hase

Frankfurt  iliyofikia  fainali msimu  uliopita  itakwaana  na  FC Heidenheim  ya  daraja  la  pili. SC Paderbon ambayo  ni  timu pekee  ya  daraja  la  tatu  iliyobakia  katika  kinyang'anyiro  hicho , inaisubiri FC Ingolstadt  ya  daraja  la  pili.  Michezo  hiyo  ya  robo fainali  inatarajiwa  kufanyika  kati  ya  tarehe 19 na  20  mwezi Desemba.

 

Mwandishi: Sekione Kitojo / dpae / rtre / afpe  / ape

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahaman