1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Marekani laidhinisha fedha kwa Afghanistan

28 Julai 2010

Bunge la Marekani limeuidhinisha mswada utakaoufanikisha mkakati wa Rais Obama wa Marekani wa kuiongeza idadi ya wanajeshi wa Afghanistan kwa alfu 30.

https://p.dw.com/p/OWLk
Rais Obama na Rais Hamid KarzaiPicha: AP

Idhini hiyo imetolewa wakati ambapo kiongozi huyo wa  Marekani anaandamwa na kashfa ya hati za siri  za kijeshi zilizovuja  kadhalika upinzani  kutoka  kwa  wanasiasa wa chama chake cha Demokratik.Wanasiasa wengi  wa chama cha Republik ndio waliouidhinisha mswada huo.Baraza la Senate lilishatoa  ridhaa yake na anasubiriwa  Rais Obama kuutia saini.Bunge hilo  la Marekani lililo na wanasiasa wengi wa Chama cha Rais Obama cha Demokratik limeuidhinisha mswada huo baada ya kusuasua kwa kipindi cha  miezi sita.Baraza la wawakilishi liliudhinisha  mswada huo kwa kura 308 na kupingwa  kwa 114.Mswada  huo  utakiruhusu kiasi cha dola  bilioni 37 kutumiwa kupambana na wapiganaji wa Taleban nchini Afghanistan.Ifahamike kuwa wengi ya waliouidhinisha mswada huo ni wanasiasa wa Republik  na wala sio wa  chama chake cha Demokratik.Jumla ya  wanasiasa 102 waliupinga mswada huo.Baraza  la Senate tayari lilishauidhinisha mswada  huo unaosubiri kutiwa saini na Rais Obama.

Republik mstari  wa mbele      

Mswada huo umezua mgongano  mkubwa kati ya wanasiasa wa Demokratik.Kwa upande  wake Wizara ya Ulinzi ya Marekani ,Pentagon ilitumia  mbinu zote kuhakikisha kuwa fedha hizo zinapatikana na ikajitetea kuwa endapo hilo halingefanyika ifikapo mwezi wa  Agosti,ingelazimika kuipunguza mishahara ya wafanyakazi wa kawaida  ili kuliziba pengo hilo. Wanasiasa wanaouunga mkono mswada huo walisisitiza kuwa si sahihi kuzichelewesha fedha zitakazotumiwa kuyafadhili  mahitaji  ya wanajeshi ambao tayari wameshapelekwa vitani. 

Chini ya mpango huo  mpya wa  dharura,Rais Obama ataweza kuyafadhili mahitaji ya  kupeleka Afghanistan wanajeshi alfu 30 wa ziada  vilevile baadhi ya operesheni za Iraq.Kiasi hicho cha dola bilioni 37 ni nyongeza ya dola bilioni 130 ambazo tayari zimeshaidhinishwa na Bunge la Marekani mahsusi kwa shughuli hiyo kwa mwaka huu.Kiasi cha  dola trilioni 1 kimeshatumiwa  kuzifadhili operesheni  za Afghanistan na Iraq tangu mwaka 2001.

Kashfa  ya Wiki-leaks

Yote  hayo yanatokea wakati ambapo Marekani inaandamwa na kashfa ya hati za siri za kijeshi  zilizovuja.Nyaraka hizo zilichapishwa kwenye mtandao unaofichua taarifa za siri wa Wikileaks,na zinadai kuwa wanajeshi wa Marekani  walizificha  taarifa za  vifo vya raia wa kawaida na kwamba Pakistan inawaunga  mkono wapiganaji wa Taleban ila  bado inaendelea kupokea misaada kutoka  kwa Marekani.Hata hivyo  Rais Obama aliusisitizia umuhimu  wa kuendelea  na mkakati huo hata baada ya kuvuja huko.Badala yake Rais Obama alifafanua  kuwa hakuna  jipya  lililojitokeza  kwenye taarifa hizo.Kamanda  mkuu mteule wa jeshi la Marekani,Jenerali James Mattis aliziafiki kauli hizo. 

No Flash Internationale Afghanistan-Konferenz in Kabul
Rais wa Afghanistan's Hamid Karsai (kati) na viongozi wa kimataifa walipoafikiana kuanza kuondoa vikosi vya kigeni AfghanistanPicha: dpa

Kulingana na wachambuzi,hali yote kwa  jumla  inatoa picha tofauti kwani kwa upande mmoja serikali inataka  kuungwa na mkono na umma katika hivyo  na kwa upande wa pili inajiandaa kuviondoa vikosi vyake ifikapo mwezi wa Julai  mwakani kama  alivyotangaza Rais Obama.Baadaye hii leo mjumbe maalum wa Marekani Richard Holbrooke atarakiwa kujibu  maswali mbele  ya  jopo maalum la bunge kuhusu makakati huo wa Afghanistan.   

Kwa upande mwengine,serikali ya Afghanistan inayotaka kuisimamia misaada yake ya kigeni,imeeleza kuwa  Marekani imeshindwa kupambana  na wanaowaunga  mkono  wapiganaji wa Taleban wanaoripotiwa kujificha Pakistan.  

Ngoma ya kulaumiana   

Pakistan  kwa upande  wake imeyakanusha madai hayo ijapokuwa ina uhusiano  wa  muda mrefu kati ya vitengo vyake vya ujasusi na jeshi na kundi la  Taleban.   

Vifo vya raia wa   kawaida vilivyosababishwa na wanajeshi  wa kigeni ni jambo linalozua mivutano  mikali kati ya Rais wa Afghanistan Hamid  Karzai na viongozi wa mataifa ya magharibi  wanaomuunga mkono.Kiasi  cha wanajeshi laki  moja na nusu  wanashiriki katika mapambano  hayo dhidi ya waasi.   

Mwandishi:Mwadzaya Thelma-RTRE

Mhariri:Mtullya Abdu/