1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Burkina Faso yawafukuza wanadiplomasia wa Ufaransa kwa uasi

18 Aprili 2024

Serikali ya Burkina Faso imewafukuza wanadiplomasia watatu wa Ufaransa kutoka nchini humo ikiwatuhumu kuhusika na kile ilichosema ni "shughuli za uasi".

https://p.dw.com/p/4evST
Kiongozi wa kijeshi wa Burkina Faso, Ibrahim Traore.
Kiongozi wa kijeshi wa Burkina Faso, Ibrahim Traore.Picha: Kilaye Bationo/AP Photo/picture alliance

Barua ya wizara ya mambo ya nje ya Burkina Faso iliyotumwa kwa ubalozi wa Ufaransa na kuonekana na shirika la habari la AFP imewaamuru wanadiplomasia hao watatu waondoke katika taifa hilo ndani ya masaa 48.

Tangu kuingia madarakani kupitia mapinduzi ya Septemba 2022, utawala wa kijeshi umelitenga taifa hilo la Afrika Magharibi na mkoloni wake wa zamani, Ufaransa. 

Soma zaidi: Watu 27 wauawa Burkina Faso

Aidha utawala huo umefuta pia makubaliano ya kijeshi ya mwaka 1961 kati ya nchi hizo mbili na balozi wa Ufaransa aliondolewa baada ya mapinduzi hayo.

Kulingana na chanzo cha Ufaransa, mnamo Disemba Mosi maafisa wanne wa Ufaransa walikamatwa na kushtakiwa mjini Ougadougou.

Mamlaka za Burkina Faso ziliwataja wanne hao kama "mawakala wa ujasusi", lakini chanzo kimoja kwenye ubalozi wa Ufaransa kilisema walikuwa ni "wahudumu wa mfumo wa teknolojia ya mawasiliano."