1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMamlaka ya Palestina

Upi msimamo wa China katika vita vya Israel na Hamas

Angela Mdungu
10 Novemba 2023

China inafanya juhudi za kusuluhisha vita kati ya Israel na Hamas. Beijing imeshatoa tamko la kulaani mashambulizi yaliyofanywa na pande zote mbili katika vita hivyo, lakini umma unaonesha wazi kuchukizwa na Israeli.

https://p.dw.com/p/4YfmI
Rais wa China Xi Jinping
Rais wa China Xi JinpingPicha: Mark Schiefelbein/AP Photo/picture alliance

Hoteli ya Peace yenye jengo refu linaloonekana hata mtu akiwa katika kingo za mto Huangpu mjini Shanghai imeshawahi kuwa mwenyeji wa wageni wa serikali ya China. Miongoni mwao ni waliowahi kuwa marais wa Marekani Ronald Reagan na Bill Clinton bila kusahau watu maarufu wengine kama vile  Charlie Chaplin na George Bernard Shaw.

Ambacho wengi hawakifahamu ni kuwa jengo hilo lililojengwa na mfanyabiashara wa Kiyahudi Victor Sassoon mwaka 1929 — liliitwa the Cathay Hotel hadi mwaka 1949. Lilikuwa refu Zaidi katika mji huo kwa miaka kadhaa.

Sassoon alihamia  Shanghai miaka ya 1920s na kukuza ngome yake ya biashara mjini humo.  Wakati wa vita vya pili vya dunia, aliunga mkono ujenzi wa makaazi ya ukubwa wa kilomita 2.5 za mraba mahali ambapo wayahudi waliokuwa wakikimbia mateso ya utawala wa kinazi walijihisi kuwa salama.

Israel yakubali kusitisha mashambulizi kwa saa kadhaa Gaza

Lakini baada ya vita na Wakomunisti kuingia mamlakani China, Wayahudi wengi waliondoka Shanghai. Victor Sassoon alilazimika kuuza makampuni yake kwa chama cha Kikomunisti cha China  na kupewa kiasi kidogo cha fedha.

Kisa cha Sassoon kinaonesha chuki ambayo Wakomunist walikuwa nayo dhidi ya Wayahudi na baadaye kwa taifa lililoundwa baadaye la Israel. 

Wakati wa vita baridi, China mara zote ilitangaza kuwa iko pamoja na washirika wake wa mataifa ya Kiarabu na mara nyingi ilipiga kura dhidi ya Israeli katika Umoja wa Mataifa. Kwa hakika China haikuwa na mahusiano ya kidiplomasia kabla ya mwaka 1992 ilipoamua kuyaanzisha.

China yaiona Israel kama mshirika wake wa kibiashara

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu Picha: Abir Sultan via REUTERS

Tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia, imekuwa ikiiona Israel kama mshirika wake wa kibiashara. Kwa mwaka huu hadi sasa pande zote zimeshafanya biashara ya bidhaa zenye thamani ya fedha zisizopungua dola za Kimarekani bilioni 22.

Jeshi la Israel lakabiliana na wanamgambo wa Hamas huko Gaza

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alitarajiwa kufanya ziara China mwezi Oktoba. Moja ya ajenda kuu katika ziara hiyo ilikuwa makubaliano ya biashara huria kati ya mataifa hayo.

Ziara hiyo hata hivyo iliahirishwa baada ya mashambulizi ya kundi la Hamas  dhidi ya Israel Oktoba 7.  Nyaraka rasmi kutoka kwa Israel na China zinajikita zaidi kwenye uchumi na biashara. Hayataji sana mzozo wa Mashariki ya Kati.

Pia China imekuwa ikiiona kama mshirika mkubwa wa Marekani, wakati Marekani ni hasimu mkubwa wa Beijing. China iliyokalia kiti cha baraza la usalama la Umoja wa Mataifa mwezi Novemba kupitia Balozi wake katika Umoja wa Mataifa Zhang Jun ilisema kuwa inatoa wito kwa nchi fulani yenye ushawishi kwa pande husika kuweka kando maslahi binafsi na kufanya kila juhudi ili kumaliza vita na kurejesha amani.

Zhang alikuwa akiizungumzia Marekani ambayo ameituhumu kuwa ina maslahi yake katika vita vinavyoendelea kati ya Israel na Hamas. Hata hivyo serikali ya Beijing inadai kwamba haiegemei upande wowote kwatika mzozo huo wa Mashariki ya kati.

Scholz aahidi kuwalinda Wayahudi dhidi ya vitendo vya chuki

Beijing imekuwa na mjumbe maalumu Mashariki ya kati tangu mwaka 2019 Mwanadiplomasia huyo amepewa jukumu la kuhamasisha kuhusu amani kati ya Israel na majirani zake wa Kiarabu. Tangu kuanza kwa vita kati ya Israel na Hamas, mjumbe wa sasa Zhai Jun amekuwa akiwasiliana na washirika kadhaa pamoja na mataifa ya kiarabu. Amesema kuwa China inasimama upande wa amani na inaona kuwa "kushindwa kulinda haki za watu wa Palestina" kuwa ndiyo chanzo cha mzozo unaoendelea.

Mzozo wa Mashariki ya Kati wakaribia mwezi mmoja