1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China yaripoti maambukizi mapya 46 ya virusi vya corona

Sekione Kitojo
26 Julai 2020

China imeripoti kesi mpya za maambukizi ya virusi vya corona katika  China bara  Julai 25, ikiwa  ni ongezeko  kutoka  kesi 34 siku moja kabla, tume  ya  afya  imesema leo Jumapili(26.07.2020).

https://p.dw.com/p/3fvCi
China Corona-Pandemie | Sinopharm
Picha: picture-alliance/Photoshot

 

Miongoni mwa  maabukizi  hayo  mapya, 22 yalikuwa  katika  jimbo  la  magharibi  ya  mbali la  Xinjiang, kwa mujibu wa  taarifa  iliyotolewa  na  tume ya  taifa  ya  afya.

Hongkong | Coronavirus | Passanten mit Mundschutz
Baada ya shughuli kuruhusiwa kuendelea nchini China nchi hiyo imetangaza maambukizi mapya yanayoongezekaPicha: picture-alliance/dpa/abaca/T. Keith

China iliripoti kesi mbili mpya za watu walioonesha dalili, ikiwa  ni chini kutoka  watu 74  siku moja  kabla.

Hadi Jumamosi, China  bara  ilikuwa  na  kesi  za  maambukizi ya virusi  vya  corona  83,830 zilizothibitishwa, mamlaka hiyo  ya afya  imesema. Vifo  kutokana  na  COVID-19 vimefikia jumla  ya  watu 4,634.

Marekani  siku ya Jumamosi (25.07.2020) ilirekodi maambukizi  mapya  ya watu 68,212 katika  masaa  24 yaliyopita, chuo kikuu  cha  Johns Hopkins  kiliripoti  katika  hesabu  zake za  kila  siku. Hii  inafikisha  jumla  ya  idadi  ya  kesi  za  maambukizi  katika  taifa  hilo lililoathirika  zaidi  duniani  kufikia  4,174,437, chuo  hicho  kikuu  mjini  Baltimore kimesema leo Jumapili (26.07.2020).

Vifo vingine 1,067 viliripotiwa , na  kufikisha  idadi  ya  vifo  katika  nchi  hiyo  kuwa 146,391. Baada  ya  kupungua  katika  viwango  vya  maambukizi mwishoni  mwa  robo  ya  kwanza  ya mwaka  huu, Marekani  imeshuhudia  ongezeko  la  maambukizi  ya  virusi  vya  corona, hususan  katika  majimbo  ya  kusini  na  magharibi  mwa  nchi  hiyo  kama Califonia, Texas, Alabama na  florida.

USA Präsident Trump
Rais Donald Trump akizungumza wakati wa kutoa taarifa za maambukizi ya virusi vya corona katika Ikulu ya nchi hiyo White House Julai 22, 2020Picha: Reuters/L. Millis

Katika  siku 12  zilizopita, idadi ya  maambukizi  mapya  yanayoripotiwa  kila  siku  imepita 60,000. Wanasayansi  wanakubaliana  kuwa  ongezeko  katika  viwango  vya  vifo  linafuatia ongezeko  la  maambukizi  kwa  wiki  tatu  hadi  nne. Idadi  jumla  ya  vifo  kila  siku kwa  siku nne  zilizopita imepindukia  1,000.

Korea kaskazini

Wakati  huo  huo Maafisa  nchini  Korea  kaskazini wameweka vizuwizi vya  kuwataka  watu wasalie  majumbani  mwao  katika  mji  wa  mpakani  wa  Kaesong baada  ya  kugundua  kile walichokiita  kesi  ya kwanza ya mshukiwa  wa virusi  vya  corona, vyombo  vya  habari  vya serikali vimeripoti leo Jumapili,(26.07.2020).

Kiongozi wa nchi  hiyo Kim Jong Un aliitisha  kikao cha  dharura  cha  kamati ya  uongozi jana  jumamosi (25.07.2020) kutekeleza  "utaratibu wa dharura wa  kiwango cha juu  na kutoa  tahadhari ya kiwango  cha  juu" kudhibiti virusi, shirika  rasmi  la  habari  nchini humo KCNA lilisema.

Nordkorea I Dringlichkeitssitzung des Politbüros des WPK-Zentralkomitees
Kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un (wa tatu kutoka kushoto) akiongoza kikao maalum cha kamati ya uongozi kuzungumzia maambukizi ya virusi vya coronaPicha: Reuters/KCNA

Iwapo itathibitishwa , itakuwa  ni kesi  ya  kwanza  inayotambuliwa  rasmi  ya  COVID-19 katika  taifa  hilo  la  Korea  kaskazini ambako miundo mbinu  ya  hospitali inaonekena kuwa na  mapungufu  makubwa  kupambana  na  janga hilo.

KCNA imesema  mtu  mmoja  aliyeikimbia  nchi  hiyo  ambaye  aliondoka  na  kwenda Korea  kusini  miaka mitatu  iliyopita alirejea  Julai 19 baada  ya "kuvuka na  kuingia  nchini humo  kinyume  na  sheria" katika  mpaka wenye  ulinzi  mkali  unaogawanya  nchi  hizo mbili.Lakini  hakuna  ripoti  upande  wa  kusini wa mtu  yeyote  aliyeondoka kupitia  kile ambacho  ni  mpaka  wenye  ulinzi  mkali  kabisa  duniani, uliowekwa  mabomu ya  kutegwa ardhini  na  vituo  vya  ulinzi.