1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Clinton ashinda South Carolina kabla ya "Jumanne kuu"

28 Februari 2016

Mgombea wa urais anayewania kuteuliwa na chama chake cha Democratic nchini Marekani Hillary Clinton amepata ushindi mkubwa dhidi ya hasimu wake Bernie Sanders katika jimbo la South Carolina jana Jumamosi (27.02.2016).

https://p.dw.com/p/1I3c2
USA Vorwahl Demokraten in South Carolina - Sieg Hillary Clinton
Hillary Clinton akiwasalimia waungaji wake mkono mjini ColumbiaPicha: Reuters/J. Ernst

Na ushindi huo unamwelekeza katika siku muhimu wiki ijayo , ijulikanayo kama "Jumanne kuu" ambapo majimbo 11 yatapiga kura.

Ushindi huo unaimarisha hadhi ya Clinton kama mgombea ambaye yuko mbele katika njia ya kuweza kupata kuteuliwa na chama chake kwa ajili ya uchaguzi wa hapo Novemba 8 mwaka huu katika azma yake ya kuwa rais wa kwanza mwanamke nchini marekani.

USA Vorwahl Demokraten in South Carolina - Anhänger Hillary Clinton
Mashabiki wa Clinton wakimshangiriaPicha: Reuters/R. Hill

Vituo mbali mbali vya televisheni vimeyaita matokeo hayo kwa Clinton mara tu baada ya kukamilishwa kwa upigaji kura, na kudokeza kwamba ni ushindi mkubwa. Matokeo ya awali yanaonesha akiwa ameshinda kwa kiwango kikubwa katika maeneo mengi.

Ushindi wa waziri huyo wa zamani wa mambo ya kigeni umeonesha nguvu zake miongoni mwa wapigakura wenye asili ya Afrika, ikiwa ni sehemu muhimu ya chama cha Democratic ambao wanafanya zaidi ya nusu ya wapiga kura wa awamu hii ya mchujo katika jimbo la South Carolina.

Matokeo mazuri ya tatu

Matokeo hayo ni ya tatu kwa Clinton katika majimbo manne ya mwanzo kugombaniwa na wagombea wa chama cha Democratic, na yamezusha maswali zaidi juu ya iwapo Sanders , seneta msoshalist wa chama cha Democratic kutoka jimboni Vermont, ataweza kupanua uungwaji wake mkono kupindulia ngome yake ya wazungu ambao ni waliberali.

USA Vorwahl Demokraten in Nevada - Sieg Hillary Clinton
Clinton akisalimiana na wapiga kura wanaomuunga mkonoPicha: Reuters/D. Becker

"Leo mmetuma ujumbe," Clinton ameliambia kundi la waungaji wake mkono wakishangiria mjini Columbia baada ya matokeo kutangazwa. "Nchini Marekani , wakati tukisimama pamoja, hakuna kikwazo kikubwa ambacho hatutaweza kukivunja."

Sanders amekiri kushindwa mapema usiku huo wa Jumamosi.

"Lazima niwe muwazi katika jambo moja leo. Kampeni hii ndio kwanza inaanza. Tumeshinda ushindi muhimu New Hampshire. Ameshinda bila ubishi South Carolina. Sasa ni wakati wa "Jumanne kuu," Sanders amesema katika taarifa.

USA Vorwahl Demokraten in Nevada - Niederlage Bernie Sanders
Bernie Sanders anayepambana na ClintonPicha: Reuters/J. Young

Mpambano unazidi kupanuka

Mbio za chama cha Democratic sasa zinakuwa mpambano mpana wa kitaifa. Majimbo 11, ikiwa ni pamoja na sita upande wa kusini yakiwa na idadi kubwa ya jamii za wachache ambako maoni ya wapiga kura yanaonesha Clinton anaongoza kwa kiwango kikubwa, watapiga kura katika Jumanne kuu na majimbo manne zaidi yatapiga kura mwishoni mwa juma.

"Kesho kampeni hii inageuka ya kitaifa," Clinton amesema.

Kambi ya Clinton ilikuwa na matumaini ya ushindi mkubwa South Carolina, baada ya ushindi mwembamba katika jimbo la Iowa na Nevada na ushindi wa wazi wa Sanders katika jimbo la New Hampshire, utamuweka Clinton katika hali ya kutarajia ushindi mkubwa siku ya Jumanne, wakati kiasi ya wajumbe 875 watapiga kura zao, zaidi ya theluthi moja kati ya wajumbe hao watahitajika ili kushinda nafasi ya uteuzi.

USA Vorwahl Demokraten in Nevada - Hillary Clinton
Hillary Clinton akihutubia mkutano wa kampeniPicha: Reuters/D. Becker

Sanders, ambae ameutia nguvu upande wa Waliberali katika chama hicho na kuwavutia vijana kupiga kura kwa ujumbe wake wa kushambulia uwiano wa mapato na kukaripia biashara ya soko la hisa la Wall Street, anahitaji kushinda katika jimbo muhimu katika wiki chache zijazo ili kuweka matumaini yake hai.

Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre

Mhariri: Yusra Buwayhid