1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CONAKRY : Vyama vya wafanyakazi vyamaliza mgomo

28 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCXK

Viongozi wa vyama vya wafanyakazi wametangaza leo hii kwamba wamemaliza mgomo wao wa taifa wa siku 17 nchini Guinea baada ya kufikia makubaliano na serikali ambapo kwayo wamekubali kumchaguwa waziri mkuu mpya atakayeongezewa madaraka.

Kiongozi wa mojawapo ya vyama vikuu vya wafanyakazi nchini Guinea Ibrahim Fofana ametowa tangazo hilo lililorushwa hewani moja kwa moja na radio.

Mgomo huo uliotishwa na vyama vya wafanyakazi hapo Januari 10 uligeuka kuwa maandamano ya upizani mitaani na kugharimu maisha ya watu 59 na kusitisha shuguli zote za kiuchumi za nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Rais Lansana Conte pia amekubali kupunguza bei za bidhaa muhimu ikiwa ni pamoja na mchele na mafuta ambazo zilikuwa zimepanda mno katika miezi ya hivi karibuni.

Maandamano hayo yaliingia katika hatua mbaya hapo Jumatatu wakati vikosi vya usalama vilipowafyetulia risasi waandamanaji waliokuwa wakivurumisha mawe waliokusanyika katikati ya jiji na kujaribu kuelekea jumba la rais wakidai kujiuzulu kwa Conte.