1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Congo: Mgonjwa wa mwisho wa Ebola atoka hospitali

Saleh Mwanamilongo
4 Machi 2020

Hakuna kisa chochote cha Ebola kilicho thibitishwa nchini Congo,baada ya kupona kwa mgonjwa wa mwisho alielazwa hospitalini mji wa Beni.

https://p.dw.com/p/3YqEJ
Muuguzi akipima halijoto vipimo ya mwanamama mjini Goma,mji mkuu wa jimbo la Kivu ya Kaskazini, Mashariki mwa Congo ambako ugonjwa wa Ebola uliripotiwa toka tarehe 1 Agosti 2018.
Muuguzi akipima halijoto vipimo ya mwanamama mjini Goma,mji mkuu wa jimbo la Kivu ya Kaskazini, Mashariki mwa Congo ambako ugonjwa wa Ebola uliripotiwa toka tarehe 1 Agosti 2018.Picha: Reuters/O. Acland

Hakuna kisa chochote cha Ebola  kilicho thibitishwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, baada ya kupona kwa mgonjwa wa mwisho alielazwa hospitalini katika mji wa Beni ulio kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo.

Kiongozi wa kikanda wa shirika la afya ulimwenguni WHO, Dr Mathsidiso Moeti alielezea kwenye ekaunti yake ya twitta kwamba wamepokea kwa ''tahadhari matarajio ya matokeo mazuri'' hayo kuhusu ugonjwa huo uliotangazwa rasmi tarehe mosi Agosti 2018.

 Ugonjwa wa Ebola nchini Kongo utatangazwa kuwa umemalizika endapo hakutokueko na kisa kipya kwa muda wa siku 42.

Jumatano ya leo (04.03.2020) ni siku 15  ambayo hakujaorodheshwa kisa kipya cha ugonjwa huo wa Ebola kwenye majimbo ya Kivu ya Kasakazini na Ituri, ilielezea taarifa ya wizara ya afya ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Wauguzi wa Ebola mjini Beni, jimboni Kivu ya Kaskazini, Congo
Wauguzi wa Ebola mjini Beni, jimboni Kivu ya Kaskazini, CongoPicha: picture-alliance/dpa/Al Hadji Kudra Mliro

Matumaini ya kutokomeza Ebola

Mgonjwa wa mwisho aliyepona aliondoja jana kwenye kituo cha matibabu ya Ebola cha Beni, eneo la mwisho lililokumbwa na ugonjwa huo mashariki mwa Kongo. Mwanamama huyo Masika Mawasu Semida, alipongeza wauguzi kwa huduma aliyopewa.

''Shirika la WHO litaendelea kuunga mkono serikali ya Kongo katika kuboresha mfumo wake wa afya kwa ngazi yote'' alisema msemaji wa shirika hilo mjini Kinshasa, Mory Keita.

Watu 2,264 walikufa kutokana na Ebola  huko Beni na Ituri, ambao ni kwa mara ya kumi Kongo kukumbwa na ugonjwa huo hatari toka mwaka 1976.

 Mwezi Februari mwaka huu, kisa kipya cha Ebola kiliripotiwa baada ya siku 23 bila kisa kingine kutangazwa, hali iliyopunguza matarajio mazuri ya viongozi katika kuutokomeza ugonjwa huo. Tofauti na sasa, wakati huo kulikuwa na maeneo mengine kadhaa ambako ugonjwa huo uliripotiwa.

Watu wapatao 320.000 walipewa chanjo dhidi ya Ebola. Mwezi Julai, shirika la WHO lilitangaza ugonjwa huo wa Ebola  kuwa dharura ya kiafya ulimwenguni ,wakati huo ukitishia nchi jirani za Uganda na Rwanda.