1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

England kuvaana na Marekani nusu fainali

1 Julai 2019

Kombe la Dunia kwa wanawake limefikia hatua ya nusu fainali. Baada ya kuwalaza Ufaransa katika robo fainali Marekani ambao ndio mabingwa watetezi watapambana na England hapo Jumatano.

https://p.dw.com/p/3LPzh
FIFA Frauenfußball WM 2019 Frankreich - USA
Picha: Reuters/B. Tessier

 England wao walifuzu baada ya kuwaduwaza Norway mabao matatu bila jawabu katika mchuano wa robo fainali.

England wanastahili kutahadhari mbele ya mshambuliaji wa Marekani Megan Rapinoe mwenye miaka 33 ambaye amewasaidia kupata ushindi kwenye mechi zao mbili zilizopita.

Fußball Frauen WM in Frankreich 2019 Viertelfinale Norwegen - England
Wachezaji wa England wakisherehekea bao dhidi ya Norway kwenye robo fainaliPicha: Reuters/B. Szabo

Rapinoe alifunga mabao mawili kwenye mechi ya hatua ya timu kumi na sita bora dhidi ya Uhispania kisha katika robo fainali walipopambana na wenyeji Ufaransa alifunga mabao mengine mawili pia.

Kwenye nusu fainali ya pili ambayo itachezwa huko Lyon, Uholanzi watakuwa wanazipiga na Sweden. Sweden hapo Jumamosi waliwashangaza Ujerumani waliokuwa wamepigiwa upatua kusonga mbele walipowabandua kwa kuwafunga mbili moja.

Uholanzi nao walifika hatua hiyo ya timu nne bora baada ya kuwazidi kete Italia mabao mawili bila hata la kufutia jasho.

Fainali ya kombe hilo la dunia itachezwa huko huko Lyon siku ya Jumapili.