1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Haiti yakumbwa na tetemeko kubwa la ardhi, maelfu yahofiwa kufa

Aboubakary Jumaa Liongo13 Januari 2010

Tetemeko kubwa la ardhi limeupiga mji mkuu wa kisiwa cha Haiti, Port-au-Prince na kusababisha majengo kadhaa kuanguka na kuwafukia wakazi wa mji huo.

https://p.dw.com/p/LUNU
Moja ya majengo yaliyobomolewa na tetemeko la ardhi katika mji mkuu wa Haiti Port-au-PrincePicha: AP
<

Mawasiliano katika mji huo yamekatika kutokana na tetemeko hilo linalokadiriwa katika kipimo cha cha 7.0.

Balozi wa Haiti nchini Marekani Raymond Alcide Joseph amesema kuwa makaazi ya rais ni miongoni mwa majengo yaliyoharibiwa na tetemeko hilo, ambalo hapo awali ilidhaniwa kuwa ni Tsunami.Amesema rais wa nchi hiyo yuko salama.

´´Nimezungumza na mwakilishi wa Haiti katika jimbo la Miami Florida, bwana Ralf Lotochi, na ameniambia kuwa amezungumza na mke wa rais bibi Elizabeth Depros Prevao, na amemwelekeza aiambie dunia kuwa rais yuko salama, lakini makaazi yao yameharibiwa pamoja na jengo la wizara ya biashara´´alisema

Balozi huyo wa Haiti nchini Marekani, kisiwa ambacho ni moja kati ya nchi masikini sana duniani, amesema kisiwa hicho kimekumbwa na janga kubwa.

Pia majengo ya Umoja wa Mataifa kisiwani humo yanaarifiwa kuwa yameharibiwa na tetemeko hilo.

Rais Barack Obama ametangaza kuwa nchi yake iko tayari kukisaidia kisiwa hicho cha Haiti, ambapo Waziri wa Mambo ya Hillary Clinton amesema kuwa nchi hiyo itapeleka misaada ya kijeshi na kiraia.

Erdbeben in Haiti
Madhara ya tetemeko mjini HaitiPicha: AP

Mpaka sasa hakuna taarifa zozote za watu waliyokufa ingawaje inahofiwa kuwa mamia ya watu huenda wamekufa na wengine kujeruhiwa kutokana na tetemeko hilo.

Mwandishi:Aboubakary Liongo/Reuters/CNN

Mhariri:Thelma Mwadzaya