1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hakainde Hichilema aapishwa kuwa rais wa Zambia

24 Agosti 2021

Rais mpya wa Zambia Hakainde Hichilema ameahidi leo kuujenga upya uchumi wa nchi hiyo unaoyumba na kupunguza umaskini, wakati akiapishwa kufuatia uchaguzi uliosifiwa kuwa hatua kubwa kwa mavuguvugu ya upinzani Afrika.

https://p.dw.com/p/3zQ3d
Oppositionskandidat Hichilema gewinnt Präsidentenwahl in Sambia
Picha: picture alliance/dpa/AP

Rais mpya wa Zambia Hakainde Hichilema ameahidi leo kuujenga upya uchumi wa nchi hiyo unaoyumba na kupunguza umaskini, wakati akiapishwa kufuatia uchaguzi uliosifiwa kuwa hatua kubwa kwa mavuguvugu ya upinzani Afrika. Hichilema mwenye umri wa miaka 59 pia ameapa kurejesha haki za binadamu na uhuru wa watu mambo ambayo yalikiukwa chini ya mtangulizi wake.

“Tutajenga uchumi wetu ili tuweze kuwaondoa watu wengi katika umaskini kuliko ilivyokuwa”, alisema Hichilema alipohutubia umati wa wafuasi wake wa chama cha United Party for National Development.

Katika jaribio lake la sita la kuwania urais Hichilema alimshinda rais aliyekuwapo madarakani Edgar Lungu kwa kura karibu milioni moja.

Huo ni ushindi wa 17 wa upinzani katika eneo la Kusini mwa jangwa la Sahara tangu mwaka 2015. Hafla hiyo ya kuapishwa ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kikanda.

Lungu

Rais anayeondoka madarakani nchini Zambia Edgar Lungu alikiri kushindwa na kumpongeza mrithi wake ambaye pia ni hasimu wake wa muda mrefu Hakainde Hichilema kwa ushindi mkubwa alioupata katika uchaguzi uliokuwa na upinzani mkali.

Lungu aliahidi kufuata sheria na kuhakikisha ubadilishanaji mamlaka wenye amani. Katika hotuba yake ya kwanza kwa nchi, Hakainde Hichilema kwa upande wake ameukosoa utawala unaoondoka nchini Zambia akiahidi kuleta demokrasia nchini humo.

Rais Hichilema amesema yeye pamoja na wafuasi wake walikuwa wahanga wa utawala wa kikatili ila ameahidi kurejesha uhuru, amani na kuheshimiwa kwa haki za binadamu.