1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hamas yakabiliana tena na wanajeshi wa Israel mjini Gaza

12 Mei 2021

Wanamgambo wa Hamas na wanajeshi wa Israel leo asubuhi wamekabiliana tena huko Gaza, katika wakati ambapo inaelezwa kwamba kiasi watu 50 wameshauwawa kufuatia machafuko ya siku kadhaa

https://p.dw.com/p/3tIJZ
Bildergalerie Nahost Konflikt
Picha: Mahmud Hams/AFP/Getty Images

Kufikia sasa wapalestina zaidi ya 40 wameuwawa na idadi kubwa ya wengine wamejeruhiwa kufuatia mashambulizi yanayofanywa na Israel hasa katika ukanda wa Gaza. Majengo mawili ya ghorofa yameporomoshwa na mashambulizi ya anga ya Israel huko Gaza.

Hamas yafyatua zaidi ya maroketi 200 kuelekea IsraelNa Waisreal watano wameuwawa kufuatia mashambulizi ya maroketi kutoka Gaza. Israel imefanya mamia ya mashambulia kutoka angani kwenye ukanda huo wa Gaza leo jumatano majira ya asubuhi kwa saa za Mashariki ya kati huku wanamgambo wa kipalestina,wa kundi la Hamas na makundi mengine katika ukanda huo nao wakifyetua maroketi chungunzima kuelekea mji wa Tel Aviv na wa kusini wa Beersheba.

Bildergalerie Nahost Konflikt
Moshi ukionekana baada ya mashambulizi ya Israel Picha: Ibraheem Abu Mustafa/REUTERS

Mahakama ya ICC

Kufuatia hali hii ya machafuko Fatoue Bonsouda,mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya kimataifa inayoangalia kesi za uhalifu wa kivita amesema ana wasiwasi kwamba uhalifu wa kivita umefanywa na hasa kwa kutazama machafuko yanayotokea ukingo wa Magharibi,ikiwemo Mashariki mwa Jerusalem pamoja na Gaza.

Kutokana na hali inayoendelea mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya kimataifa inayoshughulikia uhalifu wa kivita ya ICC amezungumzia wasiwasi wake, kwamba  kuna uwezekano uhalifu umefanyika.

Bensouda ameandika ujumbe huo kwenye ukurasa wa Twitta leo jumatano akiongeza kusema kwamba uchunguzi wa mahakama ya ICC utatazama pande zote na ushahidi unaohusika wa pande zote kutathmini ikiwa kuna waliohusika na uhalifu,kwa mujibu wa sheria za mahakama hiyo ya kimataifa.

Itakumbukwa kwamba huko Nyuma March 3 Bensouda raia wa Gambia alianzisha uchunguzi kamili kuhusu hali kwenye maeneo yaliyonyakuliwa na Israel,kitendo kilichoikasirisha sana Israel ambayo hata hivyo sio mwanachama wa ICC,tafauti la mamlaka ya Wapalestina.

Bildergalerie Nahost Konflikt
Ofisa wa polisi wa Israel akikagua jumba lililoharibiwa karibu na Tel AvivPicha: Gil Cohen-Magen/AFP/Getty Images

Uchunguzi huo kimsingi utalenga kutazama kilichotokea katika vita vya Gaza vya mwaka 2014 lakini pia mauaji ya waandamanaji wakipalestina mnamo mwaka 2018. Jumuiya ya Kimataifa inashinikizwa kuitaka Israel ikomeshe matumizi ya nguvu.Waziri wa mambo ya nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu anasema.Mashambulizi ya jeshi la Israel- yauwa wapalestina huko Gaza

"Tunalaani kila siku mashambulizi,lakini jumuiya ya ulimwengu wa kiislamu inatarajia sisi tuchukue hatua. Mashambulio aina hii yanapaswa kukomeshwa. Tunapaswa kulinda haki za wapalestina,kwa mujibu wa sheria ya kimataifa,bila shaka", alisema Cavusoglu.

Waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson kwenye ujumbe wake aliouandika kwenye ukurasa wa Twitta muda mfupi uliopita amezitaka pande zote mbili Israel na Palestina kujizuia kutumia nguvu akisema Uingereza ina wasiwasi mkubwa na machafuko yanayoongezeka na idadi ya wanaouwawa.Kwa mujibu wa mjumbe wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mashariki ya kati,Tor Wennesland, Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa linatarajiwa kukutana kwa mara nyingine kuzungumzia mgogoro huu.

Kuna wasiwasi kwamba mgogoro huu unaweza kuelekea kwenye vita kamili na Waziri mkuu Benjamin Netanyahu ametangaza hali ya tahadhari katika mji wa Lod unaokaliwa na jamii ya Wayahudi na warabu ambako polisi imesema vurugu kubwa zilizuka katika baadhi ya sehemu za waarabu.