1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hatua za kuwaondoa raia Aleppo zakwama

Sekione Kitojo
17 Desemba 2016

Kikao cha dharura cha baraza la Usalama la Umoja wa mataifa kimeitishwa kujadili hali katika mji uliokumbwa na mapigano nchini Syria  wa Aleppo, amesema balozi wa Ufaransa katika Umoja wa Mataifa Ijumaa,(16.12.2016).

https://p.dw.com/p/2URhE
Syrien Krieg - Zerstörung & Evakuierungen in Aleppo
Raia wakijaribu kukimbia kutoka Aleppo masharikiPicha: picture-alliance/Anadolu Agency/M.E. Omer

Francois Delattre  aliwaambia  waandishi  habari  nje  ya  ukumbi  wa baraza  la  Usalama  la  Umoja  wa  Mataifa  kwamba  nchi  yake  na Ujerumani  zimeomba  kikao  hicho  cha  jana  Ijumaa. Amesema kuwa iwapo makubaliano  hayatapatikana  kuhusiana  na  usalama wa  kuwaondoa  raia  na  kuwezesha  misaada  ya  kiutu  kuingia katika  mji  huo  uliozingirwa  kwa  uangalizi  wa  wachunguzi  wa kimataifa, Ufaransa  na  washirika  wake  wanaweza  kuitisha  kikao maalum  cha  dharura  cha  wanachama  193  wa  baraza  kuu  la Umoja  wa  mataifa.

Syrien Krieg - Zerstörung & Evakuierungen in Aleppo
Majeruhi wa vita akiwasili katika upande salama wa Syria katika kivuko cha Bab al-hawa kati ya Syria na Uturuki.Picha: Getty Images/AFP/B. Kilic

Delattre  amesema Ufaransa  tayari  imeanza  kutayarisha  mswada kwa  ajili  ya kufikishwa  katika  baraza  la  Usalama.

Uondoaji  watu  kutoka  Aleppo  mashariki  umefikisha  mwisho ngome  kuu  na  muhimu  ya  waasi  nchini  Syria  na  kuwa  wakati muhimu  katika  vita  vya  wenyewe  kwa  wenyewe  nchini  humo, ambavyo vimefikisha  miaka  sita  sasa.

Juhudi  za  kuwaondoa  raia  usiku zilikwama  baada  ya   kuzuka kwa  mapambano  ya  silaha  na  kusababisha  hofu  kwamba  hatua za  amani  za  kusalimu  amri  kwa  wapinzani  katika  eneo  hilo kunaweza  kushindwa  wakati  maelfu  ya  watu  wanaaminika  kuwa bado  wako  katika  eneo  hilo.

Syrien Krieg - Zerstörung & Evakuierungen in Aleppo
Uhribifu mkubwa katika mji wa Aleppo katika kitongoji cha SalaheddinPicha: Getty Images/AFP/Y. Karwashan

Delattre  amesema  kikao  hicho  cha baraza  la  Usalama  la  Umoja  wa  Mataifa  kitajumuisha  barua  ya mratibu  wa  masuala  ya  kiutu  wa  Umoja  wa  Mataifa  Stephen O'Brien. "Tunaendelea  kupata  taarifa  za  kukanganya  juu  ya  kile hasa  kinachotokea  katika  eneo  hilo," amesema.

Majadiliano ya  kitaifa

Urusi ni  mshirika  muhimu  wa  rais Bashar al-Assad  katika  vita vyake  na  makundi  ya upinzani  ya  wasi. Balozi  wa Urusi  katika Umoja  wa  mataifa  Vitaly Churkin , amesema  jukumu  muhimu  la haraka   nchini  Syria  hivi  sasa  ni  kumaliza  shughuli  zote  za kijeshi  na  kuanza  majadiliano  kati  ya  serikali  na  upinzani.

Churkin  aliliambia  baraza  la  Usalama  la  Umoja  wa  Mataifa  jana Ijumaa  kwamba "Syria  imethibitisha  zaidi  ya  mara  moja  kuwapo kwake  tayari  kushiriki  katika  majadiliano  haya."

Waziri wa  mambo  ya  kigeni  wa  New Zealand  Murray McCully aliliambai  baraza  la  Usalama  kabla  ya  kuanza  kikao  cha faragha  kuhusu  Aleppo  kwamba  baraza  hilo  halijaweza  hadi sasa  kutimiza  majukumu  yake  ya  kuwaondoa  raia  na  kutoa msaada  wa  kiutu  katika  mji  huo.

Syrien Krieg - Zerstörung & Evakuierungen in Aleppo
Raia wanaojaribu kukimbia kutoka AleppoPicha: picture-alliance/Anadolu Agency/M.E. Omer

"Hadi  pale  hali  hiyo  itakapobadilika, mawazo  yetu  ni  kwamba kikao maalum cha  dharura  cha  baraza  kuu  la  Umoja  wa  mataifa ni  hatua  nyingine  sahihi,"  amesema.

Katibu mkuu  anasikitika

Katibu  mkuu  anayeondoka  madarakani  Ban Ki-moon  amesema Umoja  wa  mataifa  uko  tayari  kutoa  msaada  kuwaokoa  watu wengi  kadri  inavyowezekana - hata  ikiwa  operesheni  iliyofanyika usiku  imesitishwa.

Akizungumza  na  waandishi  habari  katika  kikao  chake  cha mwisho  na  waandishi  habari katika  makao  makuu  ya  Umoja  wa Mataifa  jana  Ijumaa, Ban aliita vita  nchini  Syria " vinavyonivunja moyo."

Marokko Klimakonferenz COP22 in Marrakesch
Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Ban Ki-moonPicha: picture-alliance/dpa/M. Messara

Hata  hivyo  amesema  maelfu ya  watu  wameondolewa  kutoka Aleppo  mashariki  usiku  kwa  msaada  wa  mashirika  ya  Umoja wa  Mataifa, shirika  la  msalaba  mwekundu  na hilali  nyekundu, ikiwa  ni  pamoja  na  wagonjwa  194 ambao  waliondolewa  na kupelekwa  hospitalini  katika  maeneo  mengine ya  Syria  na Uturuki.

"Nasikitika  sana  kwamba  tunalazimika  kusitisha  operesheni  hii katika  wakati  huu," alisema  katika  mkuu  Ban.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / ape

Mhariri: Bruce Amani