1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hujuma za NATO zaua raia Libya

Halima Nyanza21 Juni 2011

Jumuia ya Kujihami ya NATO imekiri kufanya mashambulio ya anga magharibi mwa mji mkuu wa Tripoli, ambalo utawala wa Libya umesema limeua watu 15. Wakati huohuo China ikimkaribisha kiongozi wa waasi wa Libya nchini humo.

https://p.dw.com/p/11g1g
Vifusi vikiondolewa katika jengo lililoteketezwa na NATOPicha: AP

Jumuia ya Kujihami ya NATO imekiri kuwa ndege zake za kivita mapema jana zilishambulia eneo la Sorman, lakini imesisitiza kuwa ililenga eneo la kijeshi.

Hata hivyo msemaji wa serikali ya Libya Mussa Ibrahimu alisema watu 15 wakiwemo watoto watatu waliuawa katika shambulio hilo, ambalo ameliita kuwa "..ni la kigaidi na haliwezi kuhalalishwa".

Libyen / Panzer / Kämpfe
Majengo yaliyoteketezwaPicha: AP

Amesema shambulio hilo lilifanywa katika shamba la mpiganaji mwenzake kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi. Lakini Kamanda wa jeshi la NATO, katika operesheni za Libya Luteni Jenerali Charles Bouchard kutoka Canada amesema walilenga katika eneo la kijeshi.

Aidha amesema popote pale Gaddafi ataficha wanajeshi wake na dhana zake anazozidhibiti, watazitafuta na kuziteketeza.

Waandishi wa habari waliotembelea eneo hilo lililoshambuliwa walishuhudia uharibifu mkubwa wa majengo katika shamba hilo la bwana Khuwildi Hemidi, ambaye aliwahi kuwa mjumbe wa baraza la uongozi la mapinduzi lililoundwa na Gaddafi wakati alipoingia madarakani mwaka 1969.

Kiongozi wa waasi ziarani China:

Wakati huohuo, China imesema mkutano wao na kiongozi wa waasi wa Libya ambaye yuko nchini humo kwa ziara ya siku mbili ni juhudi za kutafuta ufumbuzi wa haraka katika mzozo uliokumba nchi hiyo ya Afrika kaskazini.

Mahmoud Jibril Nationaler Übergangsrat Libyen
Mahmoud JibrilPicha: picture-alliance/dpa

Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la mpito Mahmoud Jibril anatarajiwa pia kukutana na Waziri wa Mambo ya nje wa China Yang Jiechi katika kubadilishana mawazo juu ya mzozo huo. Jibril aliwasili nchini China hii leo.    

Tayari maafisa wa China wameshakutana kwa mazungumzo mara mbili na viongozi wa uoinzani nchini Libya tangu ilipotangaza mwara ya kwanza kukutana kwa mazungumzo na Mostafa Abdul Jalil mapema mwezi Juni.

China pia ilifanya mazungumzo na Maziri wa Mambo ya nchi za nje wa Libya Abdul Ati Al-Obidi ambaye yuko katika serikali ya Gaddafi.

Mkutano waahirishwa:

Katika hatua nyingine, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Italia imesema mkutano mkubwa wa jumuia za kiraia za Libya uliopangwa kufanyika mjini Roma na uliopangwa pia kuwashirikisha wawakilishi wa makabila umeahirishwa.

Hata hivyo, Msemaji wa wizara hiyo amesema tarehe mpya ya kufanyika kwa mkutano huo bado haijaelezwa na kuongeza kwamba mkutano huo ulioandaliwa na wapinzani wa serikali ya Libya, ulipanga kujumuisha jamii zote za wa Libya.

Awali, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Italia, Franco Frattin alisema washiriki kati ya 200 na 300 walitarajiwa kuhudhuria mkutano huo na kuuita mkutano huo kuwa ni "baraza kubwa la maridhiano".

Mwandishi: Halima Nyanza

Mhariri: Abdul-Rahman