1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Marekani lafungua njia kwa Trump kuchunguzwa

Grace Kabogo
1 Novemba 2019

Ikulu ya Marekani imesema hatua ya Bunge la nchi hiyo kuidhinisha azimio la uchunguzi dhidi ya Rais Donald Trump unaokusudia kumuondoa madarakani haukuzingatia haki na kwamba ni kinyume na katiba.

https://p.dw.com/p/3SKN0
USA | Repräsentantenhaus | Trump | Impeachment
Picha: Getty Images/W. McNamee

Akizungumza muda mfupi baada ya azimio hilo kupitishwa, msemaji wa Ikulu ya Marekani, Stephanie Grisham amesema Trump hajafanya chochote kibaya na kwamba kitendo cha wanachama wa Democratic ni ukiukaji usiokubalika.

Kwa upande wake, meneja wa kampeni wa Rais Trump, Brad Parscale amesema wapiga kura watawaadhibu wanachama wa Democratic wanaounga mkono suala hilo na kwamba kiongozi huyo wa Marekani atachaguliwa tena kwa urahisi.

Wabunge wawili wa Democratic wapinga

Siku ya Alhamisi, Bunge la Marekani lilipitisha azimio hilo kwa kura 232 dhidi ya 196, huku wabunge wote wa chama cha Republican wakilipinga, wakiungwa mkono na wabunge wawili wa chama cha Democratic. Azimio hilo linafungua njia ya sheria za msingi za kumchunguza rais na sio kura ya kuamua iwapo wamchunguze rais au la.

Huo ni ushindi kwa chama cha Democratic ambacho ndicho kinachodhibiti uchunguzi huo katika bunge. Uchunguzi huo utaangazia iwapo Trump aliishinikiza Ukraine kwa kuweka masharti ili iweze kumchunguza mpinzani wake kisiasa Joe Biden pamoja na mtoto wake wa kiume Hunter.

Trump verkündet Tod von IS-Anführer Al-Bagdadi
Rais wa Marekani, Donald TrumpPicha: picture-alliance/AP Photo/A. Harnik

Afisa wa zamani wa ngazi ya juu wa Ikulu ya Marekani, Tim Morrison amethibitisha kuwa msaada wa kijeshi ulizuiwa na Trump kama sharti la kuitaka Ukraine ambayo ni mshirika wake kumchunguza Biden, lakini amethibitisha kwa mtazamo wake haikuwa kinyume cha sheria

Baada ya kura hiyo, Trump aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter akisema hiyo ''ni kampeni mbaya na kubwa dhidi yake katika historia ya Marekani.'' Trump ametoa wito kwa wanachama wa Republican kumuunga mkono wakati huu anapokabiliwa na kitisho cha kuondolewa madarakani. Iwapo hilo litafanikiwa, Trump atakuwa rais wa tatu katika historia ya Marekani kuondolewa madarakani na bunge la nchi hiyo.

Mwenyekiti wa Kamati ya bunge ya kijasusi, Adam Schiff amesema iwapo rais atatumia vibaya ofisi yake na kushindwa kuitetea katiba kutokana na ajenda binafsi au za kisiasa waanzilishi wa nchi hiyo waliweka utaratibu wa suluhisho ambalo ni kuchunguzwa.

Washington Adam Schiff House Intelligence Committee Vorsitz
Mwenyekiti wa Kamati ya bunge ya kijasusi, Adam SchiffPicha: picture-alliance/AP Photo/P. Monsivais

''Hii ni siku kubwa katika historia ya nchi yetu ambapo mwenendo mbaya wa rais umetulazimisha kuendelea kusonga mbele na mchakato wa kufanya uchunguzi. Azimio la leo linaainisha taratibu za kuendelea na mchakato wa uchunguzi. Hatufurahii kuchukua njia hii na kuendelea na uchunguzi, lakini pia hatuwezi kuiacha,'' alisema Schiff. Aidha, Schiff amesisitiza kuwa chama cha Democratic kitatekeleza majukumu yake kwa uzito unaostahili.

Azimio hilo litaliwezesha Bunge la Marekani kufanya mahojiano katika vikao vyake na watu mbalimbali na katika wiki zijazo mashahidi zaidi wataitwa mbele ya kamati ya bunge kutoa maelezo kuhusu madai mbalimbali yanayomkabili Trump.

Hata hivyo, wakili wa John Bolton ameonyesha ishara kwamba mshauri huyo wa zamani wa usalama wa taifa hatotoa ushahidi wowote hivi karibuni. Wabunge wa Democratic walitaka kumuhoji Bolton wiki ijayo.

Kiongozi wa walio wachache bungeni, Kevin McCarthy amesema Wademocrats wanatumia vibaya madaraka yao na wanaichafua demokrasia kwa kujaribu kumuondoa madarakani rais, kwa sababu wanaogopa hawawezi kupambana naye katika sanduku la kura.

(AP, AFP)