1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaPoland

Manusura wa "Holocaust" wawakumbuka wahanga wa mauaji

Lilian Mtono
27 Januari 2024

Kundi la manusura wa mauaji ya Wayahudi yaliyofanywa na wanajeshi wa Nazi, hii leo linaadhimisha miaka 79 ya ukombozi wa kambi ya mateso ya Auschwitz-Birkenau wakati wa Vita vya Pili vya Dunia, huko kusini mwa Poland.

https://p.dw.com/p/4bk5u
Poland | Auschwitz |
Bendera ya Israel ikiwa imepachikwa katika reli iliyoko Birkeau wakati wa maandamano ya kuwakumbuka wahanga wa mauaji ya Holocaust Picha: Wojciech Grabowski/Zuma/IMAGO

Manusura karibu 20 wa kambi mbalimbali zilizojengwa na wanajeshi hao wa Nazi wa Ujerumani karibu kote barani Ulaya wanatarajiwa kuweka mashada ya maua kwenye kuta zenye majina ya waliouawa katika kambi ya Auschwitz na kufanya sala kwenye mnara wa Birkenau.

Kwenye maadhimisho haya wanawakumbuka karibu wahanga milioni 1.1, wengi wao wakiwa Wayahudi.

Karibu Wayahudi milioni 6 wa Ulaya waliuawa na Wanazi wakati wa mauaji makubwa ya Wayahudi ama Holocaust na makundi mengine kabla na wakati wa Vita vya Pili vya Dunia.