1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel na UN zatofautiana kuhusu takwimu za msaada Gaza

Tatu Karema
10 Aprili 2024

Israel imeushtumu Umoja wa Mataifa kwa kutoa taarifa za takwimu za chini za misaada inayoingizwa katika Ukanda wa Gaza.

https://p.dw.com/p/4edUj
UNRWA
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi wa kipalestina UNRWA linaloratibu misaada yote inayoingia GazaPicha: Mahmoud Issa/ZUMAPRESS/picture alliance

Nchi hiyo imesema kwamba Umoja huo wa Mataifa unatumia mbinu mbovu inayolenga kuficha changamoto zake za usambazaji wa misaada huku shinikizo zikizidi kuongezeka dhidi ya nchi hiyo kuruhusu kuingizwa kwa misaada zaidi katika eneo hilo.

Wakati Israel iliposema kuwa malori 419 yaliingia katika ukanda wa Gaza siku ya Jumatatu, shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi wa kipalestina UNRWA linaloratibu misaada yote inayoingia Gaza, lilisema kuwa ni malori 223 pekee yaliongia katika ukanda huo siku hiyo.

Cameron awasili Washington kujadiliana Ukraine, Gaza

Tawi la jeshi la Israel linalohusika na usambazaji wa misaada COGAT pamoja na mashirika ya Umoja wa Mataifa yamesema kuwa tofauti hiyo ya idadi inatokana na njia tofauti za kuhesabu.

Hapo jana, msemaji wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu OCHA Jens Laerke, alisema kuwa takwimu za Israel zilikuwa za malori ambayo yalijazwa misaada kwa sehemu tu ili kuzingatia masharti ya uchunguzi wa kijeshi.