1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jamii za Kigypsi zinazidi kubaguliwa

P.Martin3 Januari 2009

Hali ya hatari inaibuka katika Ulaya ya Kati huku kanda hiyo ikijiandaa kwa mzozo wa uchumi na sera za itikadi kali zinazozidi kuongezeka na kuungwa mkono zikilenga jamii za Wagypsi.

https://p.dw.com/p/GRGi
Each year, the Khamoro festival of Roma culture and music begins with a traditional parade in the streets of Prague, May 31, 2007. The festival presents numerous Gypsy music groups from around the world. This year, the guests included bands from France, Germany, Russia, Eastern Europe, or as far as from India. (CTK Photo/Rene Volfik) +++(c) dpa - Report+++
Kila mwaka sherehe za utamaduni na muziki wa Wagypsi "Khamoro" hufunguliwa kwa gwaride katika mitaa ya Prague mji mkuu wa Jamhuri ya Czech.Picha: picture-alliance / dpa

Watu wa kabila la wachache la Wagypsi ndio walioathirika zaidi kutokana na kutoweka kwa haki za kijamii baada ya mfumo wa kikomunisti kusambaratika katika nchi za Ulaya ya Kati na Mashariki.

Licha ya kuwepo chuki kali dhidi ya Wagypsi katika nchi za Ulaya ya Kati, hadi hivi sasa hakuna chama cha kisiasa kilichoweza kuuvutia umma kuhusika na sera za chuki dhidi ya Wagypsi wanaosemekana kuwa waliondoka India na wakahamia barani Ulaya katika karne ya 14.Lakini sasa makundi yanayofuata sera za itikadi kali yamepata nafasi mpya ya kuhamasisha hisia za umma dhidi ya Wagypsi.

Kwani wafuasi wa mirengo ya kushoto na kulia wanajaribu kuitumia mada ya kabila hilo la wachache,kujiimarisha zaidi nje ya vyama vya kisiasa.Kwa mfano,kundi la "Walinzi wa Hungary" lililoundwa Agosti mwaka 2007 ni aina ya jeshi la wanamgambo na wanachama wake wapatao kama 2,000 hupewa mazoezi ya viungo.Kundi hilo limeahidi kuhifadhi mila za Hungary na kuwalinda raia wake.Mnamo mwezi wa Oktoba mfano huo ukaigizwa na wafuasi wa sera kali za mrengo wa kulia nchini Jamhuri ya Czech na huko kukaundwa kundi la "Walinzi wa Taifa" likiwa pia na kiasi ya wanachama 2,000.

Hayo bila shaka ni mazingira yanayochochea machafuko.Wafuasi wa sera za itikadi kali wanavituhumu vikosi vya polisi vya nchi zao kuwa vinashindwa kuwalinda raia wake dhidi ya kile kilichoitwa "uhalifu wa Wagypsi.Wakati huo huo,Wagypsi wanasema,wao pia wapo tayari kuwa na wanamgambo wao wenyewe ili kuzilinda jamii zao.Nchini Hungary asilimia 6 ya raia ni Wagypsi.

Wanasiasa katika nchi za Ulaya ya Kati na Mashariki na hasa nchini Jamhuri ya Czech,hawakutia sana maanani vitendo vya chuki vinavyowalenga Wagypsi.Kwa maoni yao,watu wa kabila hilo wanaishi kwa misaada ya ustawi wa jamii na walilindwa kupindukia kiasi wakati wa enzi ya kikomunisti.Hata hivyo,serikali katika kanda hiyo zimeahidi kuchunguza harakati za makundi hayo na hasa ya wanamgambo.Lakini makundi hayo yanajua njia ya kujiepusha na ukiukaji wa sheria.Vile vile sheria zenye kasoro humaanisha kuwa ni rahisi kwa makundi hayo kuzikwepa sheria hizo.

Isitoshe,nchini Slovakia katika mwaka 2006 chama chenye sera kali za mrengo wa kulia kilifanikiwa kuingia katika serikali ya mseto.Na tangu wakati huo,uhalifu unaochochewa na ubaguzi wa kikabila umeongezeka kwa kipeo kikubwa ikisemekana kuwa hayo ni matokeo ya serikali kuhalalisha maoni ya kuchukiwa wageni.