1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je ni nini lengo la Kim Jong Un kwa Marekani?

1 Desemba 2017

Korea kaskazini inadai kuwa makombora yake yanaweza kufikia kila kona ya Marekani. Lakini je hilo ndilo analolitaka kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un?

https://p.dw.com/p/2od3A
Nordkorea Kim Jong-Un
Picha: Getty Images/AFP/STR

Lengo lake pekee ni kudhibiti mamlaka yake madarakani, anasema, Jürgen Hanefeld anayeongoza ofisi ya mashariki mwa Asia ya kituo cha umma cha Ujerumani ARD huko mjini Tokyo nchini Japan. 

Miaka minne iliyopita wakati Kim Jong Un alipotangaza kwamba mpango wa makombora wa Korea Kaskazini utakamilishwa mwishoni mwa 2017, hakuna mtu aliyemsikiliza. Alichukuliwa kama ni mwenda wazimu au mtu asiyetabirika. Wengine walipuuza uwezo wake wa kutawala, wakijiuliza kwa muda gani angeweza kuwa mamlakani?

Na Kim alipotangaza kwamba Korea ya Kaskazini inaelekea kuwa na silaha za nyuklia miaka miwili baadaye, na kwamba alikuwa tayari kuongea na Marekani kuhusu upunguzaji wa silaha za kivita, kila mmoja alimcheka.

Hata hivyo, sasa vicheko vimepungua na kila mtu anapaswa kukabiliana na ukweli kwamba jamaa huyo anapaswa kuchukuliwa kwa uzito.

Siku ya kihistoria?

Jürgen Hanefeld
Jürgen Hanefeld anayeongoza ofisi ya mashariki mwa Asia ya kituo cha umma cha Ujerumani ARD huko TokyoPicha: NDR/Christian Spielmann

Bila shaka hakuna mtu anayejua kama makombora yake yanaweza kuisambarisha miji ya New York au Washington, DC. Lakini je tunataka kujua kweli?

Je, si itakuwa jambo la maana zaidi kutathmini hatari badala ya kukubali? Kwa hatua hii hatuwezi kujua kama jaribio la kombora la Jumatano itakumbukwa kama siku ya kihistoria lakini inawezekana.

Korea Kaskazini imejitangaza yenyewe kuwa na nguvu za nyuklia! Hiyo sio maana tu ya tishio kubwa, pia inatoa fursa.

Kila mtu anajua kwamba hata kama makombora ya nyuklia ya Korea Kaskazini yanaweza kugonga mahali popote Marekani, wangeweza tu kufanya mara moja.

Baada ya hapo hapatakuwa na Pyongyang tena, wala Korea kwa jambo hilo - Kaskazini au Kusini.

Kwa hiyo Kim anataka nini? Anataka tu kujikinga. Anataka kudhibiti mamlaka yake madarakani. Na hiyo ndiyo sababu anataka kukutana na Marekani kama taifa lenye nguvu sambamba na Marekani.

Na sio Korea Kusini, nchi ambayo Marekani inaidhibiti angalau kijeshi.

Na sio na china ambayo imekuwa ikiiunga mkono na kusitasita ikizingatia maslahi yake ya kiuchumi na mikakati wa umuhimu wa eneo hilo kwa China.

Hapana, Kim dhidi ya Donald Trump ni mchezo ambao Korea Kaskazini inawekeza fedha zake.

Hii ni kuhusu amani

Mtu anaweza kudhani ni kiburi lakini inaonekana kwa mtamazo mwengine, hakuna njia nyingine mbadala.

Trump hana uwezo wa kufanya kitu chochote – haijalishi ndege ngapi za kivita anazituma na licha ya faida kubwa ya kijeshi ya nchi yake - isipokuwa kama yuko tayari kuiweka Korea Kusini hatarini na hatimaye kusababisha kitisho cha kutokea kwa vita vya dunia ya tatu.

Je si ingekuwa bora angeweka kando kiburi chake kama rais wa marekani angeketi chini na kuzungumza na Kim badala ya kutumia mtandao wa Twitter?

Haitokuwa mara ya kwanza kwamba rais wa Marekani anakaa chini na viongozi dikteta ili kuwashawishi wajirekebishe.

Mara nyingi mikutano hiyo na viongozi hao ni kuhusu mafuta, silaha au fedha. Wakati huu ni juu ya jambo muhimu zaidi: Amani.

Mwandishi: Fathiya Omar/DW/Jürgen Hanefeld

Mhariri: Josephat Charo