1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je, Ronaldo ataipeleka Ureno 16 bora?

28 Novemba 2022

Ureno itafuzu kwenye raundi inayofuata iwapo itaifunga Uruguay katika mechi yao ya kundi H. Ureno watazikosa huduma za Danilo Perreira ambaye amevunjika mbavu na hatoshiriki tena mechi yoyote ya hatua ya makundi.

https://p.dw.com/p/4KBx7
FIFA Fußball-WM 2022 | Portugal vs. Ghana | Tor Ronaldo
Picha: Hannah Mckay/REUTERS

Hii inamaanisha kwamba Pepe mwenye umri wa miaka 39 atapewa nafasi ya kuanza kama beki wa kati kati. Iwapo Pepe atashiriki basi huenda akawa mchezaji wa pili mwenye umri mkubwa zaidi kuwahi kushiriki mechi ya Kombe la Dunia baada ya lejendari wa Cameroon Roger Milla.

Ikumbukwe kwamba Ureno ilifungwa 2-1 na Uruguay katika mechi ya Kombe la Dunia la mwaka 2018 nchini Urusi na hapa Bernardo Silva winga wa timu ya taifa ya Ureno anazungumzia hilo.

"Naweza kusema hiyo mechi ilikuwa mechi ambayo haikuwa nzuri kwa sababu Ureno walibanduliwa na Uruguay. Nafikiri Ureno ina mabadiliko mengi ya wachezaji ikilinganishwa na Uruguay na nafikiri hii ni hali ambayo inatufaa kwa njia nzuri. Tutafanya kila tuwezalo tunapocheza na Uruguay na kuhakikisha kwamba tunachukua pointi zote tatu na tufuzu kwenye raundi ya 16 bora," alisema Silva.

Kocha wa Ureno naye Diego Alonso anadai kwamba timu yake inao uwezo wa kuwafunga Ureno katika mechi ambayo timu hiyo ya Amerika Kusini ni lazima ishinde.

Fußball WM 2018 Luis Suarez
Mshambuliaji wa Uruguay Luis SuarezPicha: picture alliance/dpa/HPIC

Alonso anasema hakuna mpinzani anayestahili kudharauliwa katika mashindano haya ya Kombe la Dunia ukizingatia timu kubwa kama Ujerumani na Argentina zilipoteza mechi kwa timu ambazo hazina historia katika mashindano haya.

"Bila shaka wana timu nzuri, mbali na wachezaji wazuri walio nao wanashirikiana vyema kama timu. Wana kocha mzoefu ambaye ameweza kushinda mataji nao. Wamekuwa pamoja kwa muda mrefu na hilo ndilo linalowafanya kuwa hatari. Ila sisi pia tuna silaha zetu na mambo yetu yanayotufanya tuwe hatari pia," alisema Alonso.