1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la DRC lachukua hatamu za uongozi wa majimbo mawili

6 Mei 2021

Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo limechukua rasmi hatamu za uongozi  wa majimbo ya Kivu ya Kaskazini na Ituri kuanzia leo, kufuatia uamuzi uliochukuliwa mwanzoni mwa juma hii  na rais Felix Tshisekedi.

https://p.dw.com/p/3t437

Rais Tshisekedi alitangaza uamuzi wa kuwaweka kondo magavana na viongozi wote wakiraia kutoka majimbo yote hayo mawili kama njia moja itakayo changia kuleta amani katika maeneo hayo yanayo kumbwa na vurugu za vita kwa zaidi yamiongo miwili hivi sasa.

Hatua hii imepokelewa kwa hisia mseto na wakazi wa mikoa hiyo.

Tangu mapema asubuhi leo Alhamisi ,wakaazi wengi katika mji wa Goma walionekana wakiziganda redio zao ili kufahamu kinacho endelea  baada ya tangazo hilo lililotolewa na rais wa Congo mwanzoni wa juma hii.

Katika mkutano wa vyombo vya habari hapo jana, aliyekuwa gavana wa mkoa wa Kivu ya Kaskazini Carly Nzanzu Kasivita na ambaye nafasi yake imekabidhiwa kwa Luteni Jenerali Luboya N´kashama amedai kuridhika na hatua hii mpya ambayo huenda ikawa ni suluhu kwa matatizo yakiusalama yanayoyakabili majimbo ya ituri na kivu yakaskazini.

Wanajeshi watakuwa na mamlaka ya kufanya misako 

DR Kongo Treffen Bintou Keita und Félix Tshisekedi
Rais Felix Tshisekedi wa DRCPicha: Giscard Kusema/Kommunikationsdienst DR Kongo

Askari hawa wa FARDC wamepewa mamlaka ya kufanya misako mchana na usiku katika majumba ili kuwatenga watu walio patikana na hatia na wale wasio kuwa na makao katika maeneo yanayofanyiwa misako.

Hatua hii ambayo ni mara ya kwanza kutekelezwa hapa nchini Congo imeibua hisia mseto kwa mamia ya wakaazi waishio katika majimbo yote haya mawili.

Wakati baadhi wameelezea kuunga mkono hatua hii aliyo ichukua rais wa taifa hili Felix Tshisekedi, wengine wamedai kuingiwa na woga wakihofia kubinywa kwa haki yakujieleza katika kipindi hiki ambamo miji yote itazingirwa na jeshi pamoja na polisi.

Haya yanajiri siku chache baada ya maandamano ya wakaazi wa miji ya Beni, Butembo na Goma waliomtaka rais Tshisekedi kutekeleza ahadi yake kwa raia wa maeneo haya kwakudumisha amani na usalama  ambao kwa zaidi ya miongo miwili wamekuwa wakiishi katika hali ya wasiwasi wa vita.  

Kulingana na mamlaka  hapa nchini imebainika kuwa hali hii ya kuweka utawala wa kijeshi katika majimbo haya mawili ni ya mwezi mmoja  lakini itaendelea kutathminiwa baada ya kila wiki mbili.