1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jinsi gani serikali zitadhibiti teknolojia ya akili bandia?

15 Juni 2023

Maendeleo ya haraka katika teknolojia ya akili bandia yanatatiza juhudi za serikali za kufikia makubaliano juu ya sheria za kudhibiti tekinolojia hiyo, inayozidi kukua kwa kasi na hivo kuibua mashaka.

https://p.dw.com/p/4Sas0
Symbolfoto | KI im Nahen Osten
Picha: Jaap Arriens/NurPhoto/picture alliance

Kutokana na majadala mkali juu ya tekinolojia ya akili bandia, serikali na mashirika yanatafuta njia za kudhibiti matumizi ya tekinolojia hiyo. Nchini Uingereza mamlaka ya fedha inashauriana na taasisi nyingine ili kuboresha ufahamu wa tekinlojia hiyo ya akili bandia kwa lengo la kuleta ufanisi katika usimamizi wa sekta hiyo. Uingereza inakusudia kuyagawanya mamlaka ya usimamizi katika sekta za haki za binadamu, afya na usalama badala ya kuunda bodi mpya ya usimamizi.

China itaanzisha taratibu za kudhibiti matumizi ya tekinolojia ya akili bandia. Hayo yamefahamika baada ya bilionea Elon Musk kukutana na viongozi wa nchi hiyo katika ziara aliyofanya. China imeshazindua mswaada wa hatua za kudhibiti sayansi ya akili bandia maarufu kwa jina la Artificial Intelligence. China itayawajibisha makampuni kuwasilisha kwa mamlaka husika tathmini juu ya matumizi salama ya tekinolijia hiyo kabla ya kutoa huduma kwa wananchi. Serikali ya China imesema itaunga mkono ujenzi wa muundo wa akili bandia utakaoendana na maslahi ya jamii.

Teknolojia ya akili bandia inaelekea kuwa uhalisia duniani

Umoja wa Ulaya pamoja na Marekani zinapaswa kuanzisha mwongozo utakaoweka taratibu za usalama wakati juhudi za kutunga sheria mpya zinafanyika. Mkuu wa kitengo cha tekinolojia kwenye Umoja wa Ulaya Margrethe Vestager amesema anaamini kuwa mswaada husika unaweza kutayarishwa mnamo wiki chache zijazo.

Hivi karibuni wabunge wa Umoja wa Ulaya walikubaliana juu ya kupitisha sheria kali na walipendekeza kupiga marufuku ujasusi wa kupiga picha sura za watu. Bunge la Ulaya mnamo mwezi Juni, linatarajiwa kuipigia kura rasimu juu ya tektonlojia ya akili bandia katika Umoja wa Ulaya.

Jumuiya ya kuwalinda watumiaji ya Ulaya (BEUC) imesema yenyewe pia ina wasiwasi kuhusu ChatGPT na mitandao mingine ya kuchati ya teknolojia ya akili bandia na imetoa wito kwa mashirika mengine ya ulinzi wa watumiaji katika nchi za Umoja wa Ulaya kuchunguza teknolojia hiyo na madhara yanayoweza kutokea kwa watu binafsi.

Mkuu wa tume ya biashara ya taifa nchini Marekani Seneta Michael Bennet, alisema mnamo mwezi Mei kwamba shirika hilo limejikita katika kutumia sheria zilizopo ili kudhibiti baadhi ya hatari zinazosababishwa na teknolojia ya akili bandia kwa mfano kuitumia teknolojia hiyo kuyaongeza nguvu makampuni makubwa na udanganyifu katika kuwatoza watu.

ChatGBT | Akili bandia
Programu mpya ya ChatGBT inayoongezeka umaarufuPicha: Andreas Franke/picture alliance

Seneta Michael Bennet aliwasilisha mswada mnamo mwezi Aprili ambao ungesababisha kuundwa kwa kikosi kazi cha kuangalia sera za Marekani kuhusu teknolojia hiyo, na wakati huo huo kutambua njia bora za kupunguza vitisho vya faraghani, uhuru wa raia na haki katika mchakato mzima wa teknolojia ya akili bandia.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres mnamo Juni ,12 aliunga mkono pendekezo la baadhi ya watendaji wa teknolojia ya akili bandia la kuundwa shirika la kimataifa la linalosimamia teknolojia ya akili bandia saw ana Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki. Guterrs alibainisha kwamba ni nchi wanachama pekee ndizo zinaweza kuunda shirika kama hilo na sio Sekretarieti ya Umoja wa Mataifa. Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa pia ametangaza kuwa kufikia mwiso wa mwaka mipango ya bodi ya ngazi ya juu ya ushauri kuhusiana na teknolojia ya akili bandia ambapo itakuwa inakagua mara kwa mara usimamizi wa teknolojia ya akili bandia na kutoa mapendekezo.