1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya Geneva yaendelea

2 Februari 2016

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa Staffan de Mistura anaendeleza jukumu lake tete mbele ya mahasimu wa Syria,akitaraji maendeleo thabiti yatakapatikana kuhusiana na masuala ya kiutu ili kuimarisha juhudi za upatanishi.

https://p.dw.com/p/1HnTy
Wajumbe wa upande wa upinzani katika mazungumzo ya amani ya Syria mjini GenevaPicha: picture-alliance/dpa/S. di Nolfi

Kwanza ilikuwa zamu ya kuzungumza na ujumbe wa serikali ijumaa iliyopita,na jana ikawa zamu ya kuzungumza na upande wa upinzani:Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa Staffan de Mistura amefanikiwa kukiuka kiunzi cha mwanzo kwa kuzileta pande mbili hasimu katika meza ya mazungumzo mjini Geneva.Leo hii amepanga pia kuwapokea mbali mbali wawakilishi wa pande hizo mbili hasimu.

Hata hivyo utaratibu unaolenga kuzishirikisha pande hizo katika mazungumzo ili kufikia ufumbuzi wa kisiasa nchini Syria bado ni tete.Baada ya kukutana na de Mistura kwa muda wa masaa mawili jana,wajumbe wa upande wa upinzani wa Syria wanasema wamepokea "risala ya maana" kutoka Umoja wa mataifa,hata hivyo wanashikilia madai yao ya kuchukuliwa "hatua za kiutu."

Msemaji wa wawakilishi wa upande wa upinzani wa kile kinachojulikana kama "Kamati kuu ya Majadiliano" inayoungwa mkono na Saud Arabia,Salim el Muslat anasema:"Ni muhimu kwetu na inaonyesha kwamba jumuia ya kimataifa pia inalizingatia hilo kwa makini, yaani kuwaondoshea usumbufu wananchi wetu-hiyo ndiyo sababu tumekuja huku-tunalizungumzia hili kabla ya kuanza aina yoyote ya mazungumzo."

Madai ya kiutu yazingatiwe

de Mistura anaonyesha kuunga mkono hoja hizo.Anasema hata kama haitakuwa rahisi kuzuwia mizinga isifyetuliwe,hata hivyo juhudi za kutaka raia waachiliwe huru ,itakuwa hatua ya mwanzo itakayoonyesha kuna kinachotendeka upande wa kiutu.Mwishoni mwa mazungumzo pamoja na wawakilishi wa upande wa upinzani Steffan de Mistura alisema "Kamati kuu ya Majadiliano" imetoa hoja muhimu,ilipotaka,sambamba na mazungumzo,wananchi wa Syria wanastahili kusikia na kuona mabadiliko nyumbani."

Genf Syrien Konferenz Staffan de Mistura
Mjumbe maalum wa Umoja wa mataifa,Staffan de MisturaPicha: picture alliance/dpa/M. Trezzini

Ikionyesha ishara ya nia njema,serikali ya Syria imeridhia jana kuruhusu "kimsingi" misaada ipelekwe katika maeneo matatu yanayozingirwa ikiwa ni pamoja na Madaya.

Mkutano wa wafadhili utaitishwa alkhamisi ijayo London

Wakati huo huo mkutano wa wafadhili umepangwa kuitishwa London alkhamisi ijayo kwa lengo la kukusanya fedha kuwasaidia watu milioni 13 na nusu wanaotaabika nchini Sria pamoja pia na wakimbizi milioni nne na laki mbili wa nchi hiyo.Huo utakuwa mkutano wanne wa aina yake.

Syrien Anschlag in Homs
Shambulio la bomu dhidi ya mji wa HomsPicha: Reuters/SANA

Mwaka jana Umoja wa Mataifa na mashirika yake walitoa wito wa kupatiwa dala bilioni 8.4 kwaajili ya Syria,lakini kilichokusanywa ni dala bilioni tatu tu nukta tatu.Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron atawakaribisha viongozi zaidi ya 70 akiwemo kansela Angela Merkel wa Ujerumani,,katibu mkuu wa Umoja wa mataifa ban ki-Moon , waziri wa mambo ya nchi za nje wa China Wang Yi na waziri mkuu wa Libnan Tammam Salam.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri :Yusuf Saumu