1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Jumanne Kuu: Majimbo 15 ya Marekani kufanya uchaguzi

Grace Kabogo
5 Machi 2024

Wajumbe wanaopiga kura wa chama cha Democratic na Republican nchini Marekani wanatazamiwa kupigia kura za mchujo kuamua majina ya wagombea wa vyama vyao kwa ajili ya uchaguzi ujao wa urais utakaofanyika mwezi Novemba.

https://p.dw.com/p/4dCDk
Wajumbe wa Republican na Democratic kuamua majina ya wagombea urais
Wajumbe wa Republican na Democratic kuamua majina ya wagombea urais Picha: Loren Elliott/REUTERS

Rais wa Marekani Joe Biden na rais wa zamani Donald Trump wanapigiwa upatu kurejea tena katika kinyang’anyiro hicho.

Kura za mchujo kuwateua wagombea wa urais vya vyama vikuu viwili vya Democratic na Republican kuelekea uchaguzi wa Novemba 7, unaofahamika kama ''Jumanne Kuu'' zinafanyika katika majimbo 15 ya Marekani na eneo jingine moja la Samoa lililoko chini ya himaya ya Marekani.

Rais Biden anayewania kwa mara ya pili bila ya kuwepo upinzani mkubwa ndani ya chama chake cha Democratic anatazamiwa kupata ushindi wa wazi.

Biden ana wajumbe 206 na Trump 276

Rais Joe Biden na Donald Trump
Rais Joe Biden na Donald Trump

Takriban theluthi moja ya wajumbe wa chama cha Democratic pia watapiga kura za mchujo nchini kote siku ya Jumanne, lakini Rais Biden hakabiliwi na changamoto kubwa ya uteuzi wa ndani ya chama chake. Chama cha Democratic kinahitaji mgombea kuwa na wajumbe 1,968. Kwa sasa Biden ana wajumbe 206, na anaweza kuifikia idadi hiyo Machi 19.

Aidha, kwa upande wa chama cha Republican, uchaguzi huo wa Jumanne Kabambe huenda ukafungua njia kwa Trump kuelekea kuteuliwa kuwania urais baadae mwaka huu.

Jumatatu Trump alishinda North Dakota

Trump tayari ameshinda kwenye majimbo 10 tangu kura zilipoanza kupigwa, ikiwemo North Dakota alikoshinda Jumatatu, huku mpinzani wake Nikki Haley akiwa amejipatia ushindi wake wa kwanza siku ya Jumapili katika jimbo la Washington DC.

Ili kushinda uteuzi wa ndani ya chama cha Republican katika uchaguzi wa urais, mgombea anahitaji kupata angalau wajumbe 1,215. Kwa sasa Trump ana wajumbe 276, huku Nikki akiwa na wajumbe 43. Zaidi ya theluthi moja ya wajumbe 865 kati ya 2,429 watashiriki. Trump anaweza kushinda rasmi uteuzi huo Machi 12.

Mpiga kura akitoa kibandiko baada ya kupiga kura siku moja kabla ya 'Jumanne Kuu'
Mpiga kura akitoa kibandiko baada ya kupiga kura siku moja kabla ya 'Jumanne Kuu'Picha: Loren Elliott/REUTERS

Hata hivyo, Trump anakabiliwa na changamoto kadhaa za kisheria, ambazo amezielezea bila ushahidi, kama zinazoendeshwa kisiasa kwa lengo la kumzuia kushinda uchaguzi. Ikulu ya Marekani, White House mara kwa mara imekuwa ikukanusha kwamba haina uhusiano wowote na kesi nyingi zinazomkabili rais huyo wa zamani.

Kulingana na utafiti wa maoni, Rais Biden anafuatia nyuma ya Trump kwenye majimbo muhimu yenye mpambano mkali, yanayojulikana kwa kubadilisha matokeo kati ya Wademocrat na Warepublican.

Wakati utafiti wa maoni wa hivi karibuni zaidi uliofanywa na shirika la habari la Reuters na taasisi ya Ipsos, umeonyesha kuwa wagomboea wote wawili wana asilimia 36 katika ngazi ya kitaifa.

 

(AP, Reuters)