1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Katibu Mkuu wa UN Gutteres ahimiza makubaliano COP28

Iddi Ssessanga
11 Desemba 2023

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amewatolea mwito wajumbe kwenye mkutano kuhusu mazingira wa COP28 kufikia makubaliano ya kuondokana na matumizi ya nishati za visukuku.

https://p.dw.com/p/4a2p9
UAE Dubai COP28 |
Mkutano wa COP28 unakamilika Jumanne, Desemba 12, 2023.Picha: Thomas Mukoya/REUTERS

Shinikizo hilo la Guterres limekuja wakati mkutano huo wa kilele wa kimataifa ukielekea dakika zake za mwisho kabla ya kumalizika siku ya Jumanne.

Kiongozi huyo mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema bado kuna mianya ambayo inaleta kizuizi cha kupatikana maridhiano miongoni mwa mataifa takriban 200 yanayoshiriki mkutano huo.

Nchi wazalishaji wakubwa wa mafuta na gesi zikiongozwa na Saudi Arabia zinashikilia msimamo wao kutokubaliana na mpango wa kusitisha kabisa matumizi ya nishati za visukuku.

Rais wa mkutano huo wa COP28 ambaye pia anaongoza shirika la taifa la mafuta la Umoja wa falme za Kiarabu, mara kadhaa ameahidi kwamba makubaliano ya kihistoria yatafikiwa kwenye mkutano huo, na amezitolea mwito nchi zinazoshiriki kutafuta maridhiano na msingi wa pamoja kuhusu suala hilo la nishati za visukuku.