1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi Mkuu wa Iran ailaumu Marekani na washirika wake

Zainab Aziz Mhariri: Jacob Safari
3 Oktoba 2022

Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei amevunja ukimya na kuzungumza juu ya maandamano yanayoendelea nchini humo ambapo ameilaumu Marekani na washirika wake kwa kuyachochea maandamano hayo.

https://p.dw.com/p/4Hgwl
Iran  Ayatollah Ali Khamenei
Picha: ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Kiongozi huyo mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei amezungumza leo baada ya kunyamaza kimya kwa wiki nzima kuhusu maandamano makubwa zaidi kuwahi kutokea nchini Iran katika muda wa miaka mingi. Khamenei amezilaumu Marekani na washirika wake kwa kupanga maandamano hayo.

Kiongozi huyo mkuu wa Iran amesema amehuzunishwa sana na kifo cha msichana Mahsa Amini aliyekuwa na miaka 22 ambaye alifariki akiwa chini ya ulinzi wa polisi wa maadili wa Iran. Kifo chake ndio kilikuwa chanzo cha maandamano yaliyozagaa kwenye nchi nzima.

Kiongozi Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei
Kiongozi Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei Picha: Office of the Iranian Supreme Leader/AP/picture alliance

Vikosi vya usalama vya Iran vilikabiliana na maandamano ya wanafunzi katika chuo kikuu cha Tehran huku kukiwa na wimbi la maandamano yanayowashirikisha wanawake na mashirika ya kutetea haki za binadamu.

Soma Zaidi:Raia wa Iran waendelea kuandamana licha ya onyo la Mahakama

Iran imevishutumu vikosi vya nje kwa kuyachochea maandamano hayo, hasa Marekani na washirika wake, na wiki iliyopita ilisema raia tisa wa kigeni wakiwemo kutoka Ufaransa, Ujerumani, Italia, Uholanzi na Poland walikamatwa. Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Iran Naser Kanani amesema si desturi ya Wairan kujiingiza kwenye malumbano ya kikabila au ya kijinsia.

Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei amesema maandamano hayo yalihusisha vitendo visivyo vya kawaida kama wanawake waandamanaji walipovua hijabu zao hadharani na misikiti, mabenki na magari ya polisi kuchomwa moto.

Wanawake kwa wanaume wanashiriki kwenye maandmano nchini Iran kupinga mauaji ya Mahsa Amini.
Wanawake kwa wanaume wanashiriki kwenye maandmano nchini Iran kupinga mauaji ya Mahsa Amini.Picha: EPA-EFE

Tamko la kiongozi mkuu wa Iran amelitoa huku maandamano katika nchi nzima yakiwa yameingia katika wiki ya tatu licha ya juhudi za serikali kukabiliana na hali hiyo. Maandamano yanaendelea mjini Tehran na katika mikoa mingine pamoja na kwamba mamlaka imezuia huduma za intaneti na mitandao ya kijamii.

Soma Zaidi:Ni ipi kazi ya Polisi wa maadili wa Iran?

Mwaka mpya wa masomo umeanza na wanafunzi wameonekana wakikusanyika na kufanya maandamano katika vyuo vikuu kote nchini Iran, kulingana na video zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, wakiimba nyimbo za kuipinga serikali na kukemea hatua za vikosi vya usalama za kuwabana waandamanaji.

Vyanzo:AP/RTRE