1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kikongwe ahukumiwa miaka 2 Ujerumani

Saumu Mwasimba
20 Desemba 2022

Irmgard Furchner alikuwa karani katika ofisi ya kamanda aliyesimamia kambi ya mateso ya wayahudi na Wapoland wakati wa vita vya pili vya dunia iliyokuwa chini ya Wanazi

https://p.dw.com/p/4LDhI
Deutschland | Fortsetzung des Prozesses gegen eine frühere KZ-Sekretärin
Picha: Christian Charisius/dpa/picture alliance

Mahakama moja ya hapa Ujerumani,imemkuta na hatia na  imetowa hukumu yake katika kesi inayomuhusu mwanamke wa umri wa miaka 97.

Irmgard Furchner alishtakiwa  kwa kuwa sehemu ya mauaji yaliyofanywa na wanajeshi wa utawala wa Wanazi katika kambi ya mateso ya Stutthof, wakati wa vita vya pili vya dunia.

Mahakama ya Ujerumani imemkuta na hatia na imemuhukumu Irmgard Furchner kifungo  cha nje cha miaka miwili  kwa kuwa mshirika kwenye matukio ya uhalifu wa mauaji yaliyofanywa katika kambi ya mateso ya Stutthof iliyokuwa ikiendeshwa na utawala wa wanazi wa Ujerumani wakati wa vita vya pili vya dunia.

Shirika la habari la kijerumani dpa limeripoti muda mfupi uliopita kwamba hukumu hiyo imetolewa kwa kuzingatia maombi yaliyotolewa na waendesha mashataka.

Irmgard Furchner alikuwa msaidizi wa kamanda aliyekuwa akiisimamia kambi ya mateso ya Stutthof wakati wa vita ya pili ya dunia.

Anatuhumiwa kuwa sehemu ya vyombo vya dola chini ya utawala wa chama cha Wanazi aliyesaidia uendeshaji wa kambi hiyo ya mateso. Kesi hiyo imeendeshwa katika mahakama inayoshughulikia watuhumiwa wenye umri mdogo kwasababu uhalifu anaodaiwa kuufanya Furchner wakati huo alikuwa na umri wa chini ya miaka 21.

Mauaji ya kambi ya Stutthof

 Katika kesi hiyo mtuhumiwa anadaiwa alikuwa mshirika aliyewasaidia na kuwachochea waliokuwa wakiisimamia kambi ya mateso ya Stutthof kuendesha mauaji yaliyopangwa makusudi ya watu waliofungwa kwenye kambi hiyo kati ya mwezi Juni mwaka 1943 na Aprili mwaka 1945.

Kazi aliyokuwa akiifanya  Bibi Furchner ni ya ukarani na mpiga chapa katika ofisi ya kamanda wa kambi hiyo.

Mawakili wanaomtetea mtuhumiwa huyo waliomba mteja wao afutiwe mashtaka wakitowa hoja kwamba ushahidi haujaonesha waziwazi kwamba Furchner alikuwa akifahamu kuhusu mauaji yaliyokuwa yakiendeshwa kwenye kambi hiyo,na maana yake ni kwamba hakuna kinachoonesha alikuwa na nia ya kuhusika na uhalifu.

Irmgard F.
Picha: Bundesarchiv

Taarifa ya mwisho ya mtuhimiwa wakati akisikilizwa katika kesi hiyo aliomba msamaha kwa kilichotokea na kujutia kuwepo kwake katika kambi hiyo ya mateso ya Stutthof wakati huo ulipofanyika uhalifu.

Karani wa kambi ya Kinazi apandishwa kizimbani

Mwanzoni mwa kesi hii mnamo mwezi Septemba mwaka 2021 mtuhumiwa alijaribu kukwepa vikao lakini baadae alichukuliwa na polisi na kuwekwa kizuizini kwa siku chungunzima.

Kambi ya Stutthof ilikuwa kituo cha kuwakusanya wayaahudi na wapoland wasiokuwa wayahudi walioondolewa katika mji wa Danzig ambao sasa unajulikana kama Gdansk.

Polen | KZ Stutthof
Picha: Michal Fludra/NurPhoto/picture alliance

Kuanzia kama mwaka 1940 kambi hiyo ilikuwa ikitumika kama kile kilichoitwa''kambi ya mafunzo ya kazi'' ambapo watu walichukuliwa kwa lazima kufanyishwa kazi,na hasa hasa wapoland na raia kutoka nchi za iliyokuwa Soviet,walipelekwa huko kutumikia vifungona mara nyingi walikufa.

Kutoka mwaka 1944 chini ya ukandamizaji wa wanajeshi wa Hitler, maelfu ya wayahudi kutoka nchi za Baltic na  Auschwitz walikamatwa pamoja na Wapoland wakati wa harakati za kujaribu kupambana kuuangusha utawala wa wanazi katika mji wa Warsaw.