1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la Afrika: Nyota wa soka wawa mashujaa wa kitaifa

Zainab Aziz
17 Januari 2024

Katika Kombe la Afrika la 2024, wachezaji watasifiwa hata kama wamekuwa wakipata pesa zao nje ya nchi kwa muda mrefu. Kwa mashabiki, wanasoka ni ishara ya nguvu na uwezo wa bara la Afrika.

https://p.dw.com/p/4bB1t
Ivory Coast, Abidjan | Michuano ya AFCON
Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON linaanza Jumamosi nchini Ivory CoastPicha: Wikus de Wet/AFP/Getty Images

Wanasoka wa Ujerumani wenye nasaba ya Afrika hukabiliwa na changamoto ya kuchagua kati ya kuchezea timu za taifa za Ulaya na za mataifa ya Afrika. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wachezaji wawili wa Senegal. Tangu mwaka 2020 mwanasoka Ismail Jacobs wa timu ya AS Monaco amekuwa anaichezea timu ya taifa ya Senegal.

Wakati timu ya AS Monaco ilipocheza mechi na timu ya FC Toulouse katika Ligi kuu ya Ufaransa mashabiki walikusanyika  uwanjani kumshangilia kwa sauti kubwa Ismail Jacobs wa Monaco na baadaye mwenzake Krepin Diatta.

Ismail Jacobs mwenye umri wa miaka 24 amekuwa mchezaji wa taifa la Senegal tangu mwaka 2022. Baba yake anatokea Senegal na kwa hivyo Ismail anaweza kuchagua kati ya timu ya taifa ya Ujerumani na Senegal. Katika medani ya vijana, Jacobs aliichezea nchi yake ambapo alizaliwa, yaani Ujerumani na akawa bingwa pamoja na timu ya vijana ya Ujerumani.

Kandanda  Victor Osimhen - Nigeria
Victor Osimhen ni mmoja wachezaji mashuhuri wa timu y ataifa ya Nigeria.Picha: Simone Scusa/Shengolpixs/IMAGO

Soma pia: Je, michuano ya AFCON mwaka 2024 itakuwa ya ushindani zaidi?

Jacobs amesema anajivunia kuichezea Senegal. Mnamo mwaka huo wa 2022 kocha wa timu ya Senegal, Aliou Cisse  alimwita Jacobs na kumshawishi abadilishe nchi. Alifurahi sana na alizungumza na baba yake juu ya shauri hilo. Alifanya  uamuzi mara moja na alifurahi kuanza kuichezea timu ya Senegal. Jacobs anajivunia sana nasaba yake ya Afrika japo ni mara chache tu amewahi kwenda Senegal. Amefaidi utoto wake kwa kuzichezea timu za mjini Colgne na za sehemu za  karibu.

Wachezaji wengi wa Senegal watakaoshiriki kwenye mashindano ya kugombea kombe la ubingwa wa Afrika, wanachezea klabu za nje. Litakapofunguliwa dimba la mashindano hayo, mtetezi wa taji Senegal, hana mchezaji hata mmoja kutoka klabu ya nyumbani. Wanasoka wote 27 wa timu ya Senegal wanachezea klabu za nje na hasa za barani Ulaya.

Morocco: Mafanikio ya kombe la Dunia kwa machaguo ya Ulaya

Hali hiyo inajiri pia kwa timu ya Morocco yenye wachezaji wanaojivunia sana taifa lao. Katika mashindano ya kugombea kombe la dunia nchini Qatar timu ya Morocco ilishika nafasi ya nne. Hata hivyo wanasoka wake karibu wote wanachezea  klabu za nje. Wengi wao wamezaliwa barani Ulaya.

Mtaalamu wa maendeleo ya tamaduni, Kurt Wachter kutoka Austria amesema mashindano ya kandanda ya kugombea ubingwa wa Afrika AFCON, yanayofanyika kila baada ya miaka miwili ni tukio muhimu sana kwa watu wa bara la Afrika. Wachezaji wanaochezea timu za nje ya Afrika wanazingatiwa kuwa mfano wa kuigwa.

Tanzania yafuzu kushiriki fainali za michuano ya AFCON, 2024

Soma pia: AFCON itaiathiri vipi ligi kuu ya Bundesliga?

"Wanasoka stadi wa Afrika wanaochuma fedha zao nje ya nchi: Ulaya, Uarabuni, au Marekani, hakika wanaonekana kuwa mfano wa kuigwa. Hii ni kweli hasa kwa vijana wanaoweza kuwaona wanasoka hao katika ligi kuu ya Uingereza, au Paris St. Germain kupitia vyombo vya habari. Hilo linahusishwa na pesa na umaarufu. Ni nani asiyetaka kitu kama hicho?"

Hata hivyo mtaalamu huyo wa maendeleo ya tamaduni Kurt Wachter ametilia maanani kwamba wasomi barani Afrika  wanapendelea kuona mifano ya kuigwa katika tasnia za sayansi, tiba na tekinolojia. Mtaalamu huyo amesema wanasoka  hao wa Afrika ni taswira danganyifu!

Mtaalamu huyo wa maendeleo ya tamaduni amesema hakuna wivu au chuki miongoni mwa mashabiki nyumbani kuhusu utajiri au mafanikio ya wenzao, ambao wanafanya kazi kama wanasoka wa kulipwa mbali na nyumbani. Ameeleza kuwa mashabiki hao wanajivunia mafaniko ya mashujaa wao na wanawaona kuwa ni ishara ya maendeleo.