1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la Mabara latua nyumbani Ujerumani

Bruce Amani
3 Julai 2017

Mabingwa wa Kombe la Mabara Ujerumani wamerudi nyumbani, isipokuwa hakukuwa na sherehe za aina yoyote zilizopangwa kwa sababu timu hiyo inakwenda likizoni moja kwa moja.

https://p.dw.com/p/2fqtq
Nationalmannschaft zurück in Deutschland
Picha: picture alliance/dpa/A. Dedert

Licha ya kutowapeleka Urusi wachezaji wake wengi vigogo, Ujerumani ilibeba Kombe la Mabara kwa mara ya kwanza hapo jana kwa kuwafunga mabingwa wa Amerika Kusini Chile bao moja kwa bila. Na hata baadhi ya mashabiki wa nyumbani walionekana kutokuwa na imani na timu yao. Baada ya mafanikio katika Kombe la Mabara na ubingwa wa Ulaya kwa wachezaji wasiozidi umri wa miaka 21 katika kipindi cha saa 48, kocha Joachim Loew anajiskia kuwa katika mbingu ya tisa wakati akiweka mikakati ya kutetea taji la Kombe la Dunia nchini Urusi mwaka ujao.

Fußball Chile v Deutschland - FIFA Confederations Cup Russia 2017 - Finale
Ujerumani iliizaba Chile katika fainaliPicha: picture-alliance/AP Photo/T. Stavrakis

Siku mbili kabla, timu ya Ujerumani ya wachezaji wa chini ya umri wa miaka 21 walishinda taji la Ulaya, kwa kuwaduwaza Uhispania bao moja kwa bila. 

Loew mwenye umri wa miaka 57, sasa yuko katika mwaka wake wa 11 akiwa usukani, na ana kundi la zaidi ya wachezaji 40 wa kuwafuatilia wakati muda ukiyoyoma tayari kwa Kombe la Dunia. Wote wamefanyiwa majaribiwa na wana uzoefu wa mashindano makubwa. Loew alisisitiza nia yake ya kukuza vipaji "Wachezaji waliobaki nyumbani ni wazuri sana. Na bado wanacheza katika kiwango cha juu kabisa. Lakini sasa tuna kikosi mbadala.na hilo lilikuwa lengo langu la kwanza kando na kushinda Kombe hili bila shaka. Kila mara nasema suala la kipaumbele kwangu ni kukuza vipaji. Nataka kuwapa vijana nafasi za kuwa na uzeofu katika mechi za kimataifa kama hizi. Na tumeweza kufanikisha hilo. Kwa sababu wachezaji wote waliokuwa kwenye kikosi wapo katika hali nzuri sasa kuliko walivyokuwa kabla ya Kombe la Mabara

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Reuters
Mhariri: Josephat Charo