1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kongamano la kiuchumi laanza Ethiopia

9 Mei 2012

Viongozi wa kisiasa, wakurugenzi wa makampuni ya biashara na wawakilishi wa asasi za kiraia wamekutana katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa, kujadili uwezo wa ukuaji wa kiuchumi wa nchi za Kiafrika.

https://p.dw.com/p/14sNt
World Economic Forum Logo
World Economic Forum LogoPicha: picture-alliance/ZB

Mkurugenzi wa kongamano la kiuchumi la dunia, katika bara la Afrika, Bi Elsie Kanza, amesama kwamba washiriki wa kongamano la Addis Ababa wanakutana kutafuta mbinu za kuongeza kiasi cha uwekezaji katika nchi za Afrika pamoja na mbinu za kupanua uchumi wa nchi hizo ili usitegemee sekta moja tu. "Tunataka kuhakikisha kwamba maendeleo yanaboreshwa, maisha ya watu yanaboreshwa na idadi kubwa ya watu inafaidika," alisema Bi Kanza.

Zaidi ya watu 700 wanahudhuria kongamano hilo, miongoni mwao akiwa waziri mkuu wa zamani wa Uingereza, Gordon Brown, pamoja na viongozi wa kutoka nchi za Kiafrika kama vile kutoka Gambia, Ethiopia, Gabon, Nigeria, Rwanda na Tanzania.

Kofi Annan ni miongoni mwa viongozi wa kangamano la kiuchumi
Kofi Annan ni miongoni mwa viongozi wa kangamano la kiuchumiPicha: dapd

Akifafanua kuhusu mada zitakazozungumziwa katika kongamano la Addis Ababa, waziri wa mambo ya kigeni wa Tanzania, Bernard Membe, alisema: "Angalizo la kwanza katika Economic Forum ya sasa inayoanza Addis Ababa ni kuangalia ni namna gani Afrika itatunza rasilimali zake yenyewe bila ya kuziuza na kuziondoa na kuiuza au kuisaliti Afrika duniani."

Uchumi wa Afrika waendelea kukua

Mkutano huo wa siku tatu utajadili pia namna ya kuhifadhi mazingira na kuhimiza utawala bora. Washiriki watazungumzia pia namna ambavyo nchi za Afrika zinaweza kufaidika kutokana na mataifa yanayokua kiuchumi kwa kasi kama vile China. Hata hivyo Bernard Membe ametahadharisha kwamba viongozi wa Afrika watabidi kuwa makini katika kutetea bara lao hasa katika kipindi hiki kilichotawaliwa na changamoto za kiuchumi duniani.

Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Gordon Brown
Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Gordon BrownPicha: AP

Viongozi kadhaa wa kisiasa na wa kiuchumi wanaongoza kongamano hili la kiuchumi, akiwemo katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Matifa Kofi Annan na rais wa shirika la uwekezaji kutoka China liitwalo China Investment Corporation, Bw. Gao Xiqing.

Katika miaka iliyopita, uchumi wa nchi za Kiafrika umekuwa ukikua kwa kasi na inatarajiwa kwamba ukuaji huo utafikia asilimia 6 mwaka huu. Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, nchi 7 kati ya 10 zinazokuwa kwa haraka kuliko zote kiuchumi zilikuwa za Kiafrika. Kiasi cha uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nchi za nje kimeongezeka na hivyo kuukuza uchumi zaidi.

Mwandishi: Elizabeth Shoo/AFP

Mhariri: Saumu Yusuf