1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

AfD chachagua kiongozi wa kampeni uchaguzi wa bunge la Ulaya

Angela Mdungu
30 Julai 2023

Chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha Ujerumani AfD kimesema kitaingia katika kampeni za Ulaya za mwaka 2024 chini ya uongozi wa mbunge wake katika bunge la Umoja wa Ulaya Maxmillian Krah.

https://p.dw.com/p/4UYdR
Maximilian Krah, atakayeongoza kampeni za AfD kwenye uchaguzi bunge la Ulaya
Maximilian Krah, atakayeongoza kampeni za AfD kwenye uchaguzi bunge la UlayaPicha: dts Nachrichtenagentur/IMAGO

Krah ambaye ni mwanasheria mwenye miaka 46 aliidhinishwa na chama chake katika nafasi hiyo kwa asilimia 6.7 ya kura kwenye mkutano unaohusu uchaguzi katika bunge la Ulaya.

Katika kongamano la chama chicho cha AfD wajumbe walimchagua pia mbunge wa Bavaria katika bunge la Ujerumani Petr Bystron kuwa katika nafasi ya pili kwenye orodha ya wagombea wa bunge la Ulaya. Alipita bila kupingwa kwa silimia 82 ya kura.

Soma zaidi: AfD yabainisha mikakati katika mkutano wake wa mwaka

Mbunge wa Chama hicho mbadala cha Ujerumani katika bunge la jimbo la Thuringia René Aust, aliungwa mkono kwa asilimia 67.8 na kushika nafasi ya tatu.

Tawi la AfD la Thuringia linatajwa na shirika la intelijensia la ndani nchini Ujerumani kuwa lenye siasa kali na kwa sasa linafuatiliwa kwa karibu.

Mienendo yenye utata ya Krah kwenye bunge la Ulaya

Ugombea wa Krah umekuwa wa kutatanisha ndani ya chama hicho kutokana na mwenendo wake wa awali uliogubikwa na usumbufu katika bunge la Ulaya ambako amekuwa mbunge tangu mwaka 2019. Jana Jumamosi, Krah aliwatuhumu wapinzani wake ndani ya AfD kwa kufanya kampeni za miezi kadhaa za kumchafua.

Kongamano la AfD linafanyika mjini Magdeburg
Kongamano la AfD linafanyika mjini Magdeburg Picha: picture alliance/dpa

Uchaguzi huo umefanyika wakati wa mkutano mkuu wa chama uliofanyika katika mji wa Magdeburg. Katika mkutano wao unaoendelea leo Jumapili, Chama hicho kinaendelea kuchagua wagombea wengine watakaoshiriki kwenye uchaguzi wa bunge la Ulaya baada ya nafasi tano za kwanza kujazwa jana. Kinatarajiwa kutoa orodha ya wagombea 30 kwenye uchaguzi huo utakaofanyika mwezi Juni mwakani.

Hivi sasa AfD kina viti vinne kwenye bunge hilo lenye wabunge 705. Kongamano la leo la chama hicho litaahirishwa leo kwa muda kabla ya kuendelea Ijumaa.