1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ruto: Tumefuta viza kwa wageni wote wanaotaka kuingia Kenya

12 Desemba 2023

Wageni wote wanaotembelea Kenya kuanzia mwezi ujao wa Januari hawatahitaji vibali na badala yake mamlaka nchini humo imeunda mfumo wa kidigitali ambao umerahisisha mchakato kwa wasafiri.

https://p.dw.com/p/4a4yw
Diplomasia Kenya | Rais Willium Ruto
Rais wa Kenya William RutoPicha: TONY KARUMBA/AFP

 

Ruto alisema serikali yake imeunda mfumo wa kidijitali ili kuhakikisha wageni wote watapokea idhini ya usafiri wa kielektroniki mapema, badala ya kuhitaji kutuma maombi ya visa.

Hayo yamebainika kwenye hotuba ya Rais William Ruto aliyeongoza sherehe za miaka 60 ya uhuru wa Kenya kutoka kwa mkoloni Uingereza.

Alisema hakutakuwa na haja kwa mtu yeyote kutoka katika kilapembe ya dunia kuomba nyarakaya kumruhusu kuingia kenya.

"Haijalishi unatoka pembe gani ya dunia hautahitajika kubeba mzigo wa kuomba visa" Alisema

Rais Ruto kwa muda mrefu amekuwa akitetea hoja ya kusafiri bila vibali katika eneo la Afrika, hatua ambayo bado inawatia wasiwasi baadhi ya wachambuzi wa masuala ya usalama na uchumi.

Soma pia:Kenya inatafuta utulivu wa kiuchumi baada ya miaka 60 ya uhuru

Katika mkutano uliowaleta viongozi wa maaifa ya Afrika Mashariki mwezi Oktoba rais Ruto alisema watu kutoka nchi za Afrika hawangelihitaji visa kuingia Kenya kufikia mwisho wa 2023.

Mataifa jirani yahudhuria sherehe za Uhuru

Marais wa Zanzibar Dr Hussein Mwinyi na mwenzake wa Ethiopia Sahle Zewdi walihudhuria sherehe hizo ambazo ni za pili kuongozwa na William Ruto.

Naibu Waziri mkuu wa Uganda Rebecca Kadaga ambaye pia ni waziri wa masuala ya Afrika Mashariki Pamoja na naibu Rais wa Burundi Prosper Bazobanza nao pia walifika kuiwakilisha Jumuiya ya Afrika mashariki.

Naibu wa Rais wa Kenya Rigathi Gachagua aliyeandamana na mkewe Pasta Dorcas aliusisitizia umuhimu wa kudumisha Amani na ustawi wa Taifa.

Maoni na matarajio ya Wakenya kwa utawala wa William Ruto

Itakumbukwa kuwa Kenyailijinyakulia uhuru Wake kutoka kwa Koloni Uingereza mwaka 1963 na kuanza kujisimamia mwaka uliofuatia wa 1964.

Soma pia:ICC yasitisha uchunguzi machafuko baada ya uchaguzi Kenya

Kwenye ujumbe Wake, Mfalme Charles wa 3 wa Uingereza aliitakia Kenya mema na kutarajia uhusiano mwema katika siku za usoni. Ni mwaka huu huu ambapo Mfalme huyo wa Uingereza aliizuru kenya kwa Mara ya kwanza tangu kutawazwa.

Aidha Rais William Ruto aliyepongeza hatua zilizopigwa kudumisha katiba mpya ya mwaka 2010 mintarafu demokrasia.

Kauli mbiu ya sherehe za Jamhuri kwa mwaka huu ni Vijana , uchumi wa Sanaa na michezo. Ili kuipa uhai, Rais William Ruto kwenye hotuba yake alibainisha kuwa serikali imeingia ubia na kampuni ya dijitali ya Meta kuwawezesha wasanii kutumia majukwaa ya Facebook na Instagram kibiashara.