1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

IS yatangaza kifo cha kiongozi wake, yateua mpya

Iddi Ssessanga
4 Agosti 2023

Kundi la Dola la Kiislamu limetangaza Alhamis kifo cha kiongozi wake Abu al-Hussein al-Husseini al-Qurashi, ambaye limesema aliuawa katika makabiliano na kundi hasimu nchini Syria, na kumtaja mrithi wake.

https://p.dw.com/p/4Ul6J
Symbolbild islamischer Staat Fahne
Picha: CPA Media/picture alliance

Kiongozi huyo "aliuawa baada ya mapigano ya moja kwa moja" na kundi la wanajihadi la Hayat Tahrir al-Sham katika mkoa wa Idlib, msemaji wa IS alisema katika ujumbe uliorekodiwa kwenye chaneli zake kwenye programu ya ujumbe wa Telegram, bila kutaja aliuawa lini.

Msemaji huyo alimtangaza kiongozi mpya wa kundi hilo -- wa tano -- kama Abu Hafs al-Hashimi al-Qurashi.

Mwishoni mwa mwezi wa Aprili, Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan alisema kiongozi anayeshukiwa kuwa wa IS aliuawa nchini Syria katika operesheni iliyofanywa na shirika la kijasusi la Uturuki la MIT. 

"Mtu anaeshukiwa kuwa kiongozi wa Daesh, jina la kificho Abu Hussein al-Qurashi, amezimwa katika operesheni iliyofanywa ... na MIT nchini Syria," Erdogan alisema wakati huo, akitumia kifupi cha Kiarabu kwa kundi la Dola la Kiislamu.

Soma pia: Kiongozi wa ISIS Mashariki mwa Syria, auwawa na Marekani 

Vyombo vya habari vya Uturuki vilitoa picha za jengo lililozungushiwa uzio katikati ya uwanja ambapo vilisema alikuwa amejificha katika eneo la Afrin nchini Syria.

Afrin iko katika mkoa wa Aleppo -- jirani na Idlib -- katika eneo linalodhibitiwa na waasi wanaoungwa mkono na Uturuki.

Ehemaliger  IS-Chef Abu Ibrahim al-Hashimi al-Qurayshi
Picha hii isiyo na tarehe iliyopatikana kutoka CTC, ambalo ni chapisho la kituo cha kupambana na ugaidi cha West Point, linamuonyesha Abu Ibrahim al-Hashimi al-Qurayshi, kiongozi wa IS.Picha: CTC Sentinel via AP(picture alliance

Ni Uturuki au Hayat Taharir al-Sham?

Hata hivyo, msemaji wa IS alisisitiza Alhamisi kwamba Hayat Tahrir al-Sham (HTS), ambayo inadhibiti maeneo ya waasi ya mkoa wa Idlib, imemuua mkuu wa kundi hilo na kukabidhi mwili wake kwa Uturuki.

IS inaishutumu HTS -- ambayo haijadai operesheni yoyote inayomlenga kiongozi wa IS -- kufanya kazi kwa maslahi ya Ankara.

Marekani na serikali nyingine za Magharibi zimeiorodhesha HTS kama kundi la kigaidi. Shirika la habari la Uturuki la Anadolu lilisema wakati huo MIT ilifanya operesheni ya masaa manne ambapo ilimpata kiongozi wa IS.

Soma pia: Erdogan: Vikosi vya Uturuki vimemuua Kiongozi wa IS

Kiongozi wa IS alilipua fulana yake ya kujitoa mhanga alipogundua kuwa alikuwa karibu kukamatwa, Anadolu alisema, akiongeza kuwa hakuna wahudumu wa Kituruki waliouawa au kujeruhiwa.

Baada ya kuibuka kwa kishindo nchini Iraq na Syria mnamo 2014 na kuliona likiteka maeneo makubwa ya ardhi, IS ilishuhudia ukhalifa wake wa kujitangazia ukiporomoka chini ya wimbi la mashambulizi.

Utawala wa kikatili wa kundi hilo la Waislamu wa Kisunni wenye msimamo mkali na uliojaa ugaidi ulikumbwa na ukataji watu vichwa na mauaji ya watu wengi kwa kupigwa risasi.

Ilishindwa nchini Iraq mnamo 2017 na Syria miaka miwili baadaye, lakini makundi yake bado yanafanya mashambulio katika nchi zote mbili.

Mwezi Novemba mwaka jana, IS ilisema kiongozi wake wa awali, Abu Hasan al-Hashimi al-Qurashi, aliuawa.

Mtangulizi wake, Abu Ibrahim al-Qurashi, aliuawa Februari mwaka jana katika uvamizi wa Marekani katika jimbo la Idlib.

"Khalifa" wa kwanza wa kundi hilo, Abu Bakr al-Baghdadi, aliuawa, pia huko Idlib, mnamo Oktoba 2019.