1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ligi za Ulaya kurejea uwanjani mwishoni mwa juma

Sekione Kitojo
12 Oktoba 2020

Ligi za ndani katika mataifa ya Ulaya zitarejea viwanjani mwishoni mwa juma, England , Italia, Uhispania na Ujerumani

https://p.dw.com/p/3jp1i
Fußball Bundesliga Wolfsburg - Augsburg
Picha: Masterpress/Imago Images

Michezo katika  ligi  za  nyumbani  katika  mataifa  ya  Ulaya inarejea viwanjani  mwishoni  mwa  juma wakati msimu huu uliofanyiwa mabadiliko kutokana na  janga la  virusi vya corona ukiendelea kushika kasi. Nchini  Ujerumani Bundesliga  inarejea  siku  ya Jumamosi  ambapo Mainz 05 inaikaribisha Bayer Leverkusen, Hoffenheim ina miadi  na  Borussia  Dortmund, Augsburg  ina kwaana na RB Leipzig, Hertha  Berlin  inatiana kifuani  na  VFB Stuttgart, wakati  Werder Bremen  inasafiri kwenda  kupambana na  Freiburg. Timu iliyopanda daraja msimu huu ya Arminia ina miadi na  mabingwa watetezi Bayern Munich, wakati  usiku kutakuwa  na  pambano  kati ya  Borussia  Moenchengladbach ikiumana  na  VFL Wolfsburg.

Fußball Bundesliga I RB Leipzig - FC Schalke 04
Wachezaji wa RB Leipzig wakishangiria baoPicha: Jan Huebner/Imago Images

Katika Premier League nchini England Everton inamiadi katika Meryeyside derby  dhidi  ya  Liverpool, Chelsea  inacheza na Southampton, Manchester City  inapimana ubavu na  Arsenal na Manchester United  inasafiri  kwenda Newcastle. Katika  siku  hiyo hiyo katika  ligi  ya  Italia  Serie A  Juventus ni wageni wa Crotone, wakati  viongozi  wa  ligi  hiyo  hivi  sasa  Atalanta  inasafiri  kwenda Napoli. Pia  siku  hiyo  ya  Jumamosi  Real Madrid  inawakaribisha Cadiz  na  barcelona  inakibarua na  Getafe  katika  La  Liga nchini Uhispania.

Wakati huo huo katika kinyang'anyiro cha  ligi  ya  mataifa ya Ulaya , Ujerumani  itajaribu  kuendeleza  kile  ilichofanya  siku  ya  Jumamosi baada  ya  ushindi wake  wa  kwanza  kuwahi kupata  katika  ligi hiyo, inaikaribisha  Uswisi katika  kundi A4, wakati  viongozi  wa kundi  hilo Uhispania  inasafiri kwenda  Ukraine.

Baada ya mchezo  kati ya Ujerumani na Ukraine kocha wa Ujerumani  Joachim Loew  alikuwa  na  haya  ya  kusema:

"Kwa ujumla nimefarijika, kwamba tulishinda mchezo huo. Nafikiri tungeweza bila shaka  kabla ya  goli tulilofungwa na  Ukraine, kuongoza kwa mabao matatu au  manne.  Tulisababisha penalti ambayo haikuwa lazima. Kile kilichokuwa  kizuri , ni kwamba tulifanikiwa  kuwatoa nje ya mchezo Ukraine na kutoweza kabisa kutengeneza nafasi ya  kupata bao."

Joachim Löw
Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim LoewPicha: picture-alliance/dpa/P. Kneffel

Nae mchezaji wa  ulinzi  wa  Ujerumani  Matthias Ginter alikuwa  na haya  ya  kusema  kuhusu  mchezo  huo dhidi ya  Ukraine:

"Nafikiri, kwamba  tumefurahi, kwamba tumeshinda na  kwamba ilikuwa  muhimu kwa ajili  ya  kusonga mbele. Kwasababu  ushindi ndio unasaidia, na  hicho  tumefanikiwa leo , lakini tunatambua pia, kwamba  kwa sasa  hatujacheza  mchezo wa  hali  ya  juu  sana."

Siku  ya  Jumatano  Italia  itakuwa  mwenyeji  wa  Uholanzi, Ufaransa ina ziara  kwenda  Croatia katika  mchezo mwingine  wa  marudio wa fainali  iliyopita  ya  kombe  la  dunia iliyofanyika  mjini  Moscow, na mabingwa  wa  kombe  la ligi ya mataifa  Ureno  inawakaribisha nyumbani  Sweden. England  inakamilisha kipindi cha  michezo  ya kimataifa  kwa  kupambana  na  Denmark katika  uwanja  wa Wembley.

Lakini siku mbili baada  ya  Ujerumani kupambana  na  Uswisi, Bayern Munich tayari  itakuwa na  mchezo wake wa kwanza  wa baada  ya  michezo ya kimataifa. Kocha  Hans Flick  atapata fursa ya kuwa ya kuwapumzisha  wachezaji wanaorejea  kutoka  michezo ya  kimataifa  na  kuwapa wachezaji wapya  Eric Maxim Choupo-Moting, Bouna Sarr, Marc Roca na  Douglas Costa nafasi katika kikosi kinachoanza  na  kupambana  na Dueren  katika  mchezo wao wa  kombe  la  Ujerumani DFB Pokal ulioahirishwa.

UEFA Super Cup 2020 Bayern München
Kocha wa Bayern Munich Hans FlickPicha: Frank Hoermann/picture-alliance/Sven Simon

Mkutano wa kwanza  wa kikosi  kazi  cha  kitengo kinachoendesha ligi  ya  Ujerumani DFL kwa  ajili  ya  mustakabali  wa  soka  la kulipwa utafanyika  kesho  Jumanne katika  moja  kati  ya   makundi matatu, ambayo yana jumla  ya  wataalamu 35 kutoka  katika makundi  ya  kisiasa, kijamii, sayansi  na  viwanja  vya  kandanda. Wawakilishi  wa  makundi  ya  mashabiki, ambayo yanadai mageuzi katika  spoti, pia  yatajiunga  na  mkutano  huo. Kutokana  na  janga la  virusi  vya  corona Bundesliga  inakabiliwa na  shinikizo  kubwa  la kifedha.  Wakati  huo  huo  kuna  hofu ya  uwezekano wa  kugawiwa upya  fedha pamoja  na  hatua  nyingine  za  dharura ambazo zinaweza  kuathiri  uwezo  wa  vilabu  katika  mashindano  ya kimataifa.