1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maafisa wa Israel wamtaka Guterres ajiuzulu

John Juma
25 Oktoba 2023

Maafisa wa ngazi ya juu wa Israel wamemtaka Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ajiuzulu, kufuatia kauli yake kwamba mashambulizi ya kigaidi yaliyofanywa na Hamas “hayakutokea kwenye ombwe”.

https://p.dw.com/p/4Y0UA
Balozi wa Israel Umoja wa Mataifa Gilad Erdan
Balozi wa Israel Umoja wa Mataifa Gilad ErdanPicha: Mike Segar/REUTERSS

 Balozi wa Israel katika Umoja wa Mataifa Gilad Erdan alisema kuna hajya ya katibu Mkuu Antonio Guterresajiuzulu kutokana na matamshi aliyoyataja kuwa yamehalalisha ukatili wa kutisha dhidi ya watu wa Israel.

Aliongeza kwamba Umoja wa Mataifa upo kwa ajili ya kuingilia kati matendo aliyoyainisha ya kikatili kama yanayoshuhudiwa hivi sasa katika mzozo kati ya Israel na Hamas, hivyo kumsisitiza aombe radhi.

Soma pia:Israel yazidisha mashambulizi ya mabomu dhidi ya Gaza

Kwingineko msafara wa nne wa malori 20 yenye misaada umepita kivuko cha Rafah kutokea Misri kuelekea Ukanda wa Gaza mapema leo.

Khaled Zayed, mkuu wa shirika la Hilal Nyekundu la Misri tawi la Sinai Kaskazini ameliambia shirika la habari la DPA kwamba maafisa wa Hilal Nyekundu wa mamlaka ya Palestina na shirika la misaada la Umoja wa Mataifa wamepokea misaada hiyo.

Misaada hiyo ni pamoja na dawa, vyakula vya watoto na maji.

Awali, shirika la Umoja wa Mataifa lilitahadharisha kuwa upungufu wa mafuta unaweza kulilazimisha kusitisha utoaji misaada katika ukanda huo unaozongwa na vita.