1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandalizi ya Mkutano wa Kimataifa wa London juu ya Afghanistan.

Halima Nyanza22 Januari 2010

Wiki moja kabla ya kufanyika kwa mkutano wa kimataifa juu ya Afghanistan, utakaofanyika London, mataifa yanayojishughulisha na nchi hiyo tayari yameanza kupanga mikakati yake itakayoiwakilisha katika mkutano huo.

https://p.dw.com/p/Ldc9
Rais wa Afghanistan, Hamid Karzai (kushoto) na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon, wote hao wanatarajia kushiriki katika mkutano wa kimataifa kuhusu Afghanistan, utakaofanyika London Januari 28.Picha: AP

Mkutano huo wa Kimataifa utakaoijadili Afghanistan unalenga kuhamasisha maendeleo ya nchi hiyo, kuelezea kwa muhtasari mipango ya mikakati mipya ya kutilia umuhimu shughuli za kiraia katika kujenga sekta ya kilimo, kuimarisha utawala na kuwarudisha tena watu wenye misimamo mikali katika mkondo wa kiraia.

Aidha mkutano huo pia unalenga katika kuiimarisha nchi jirani na Afghanistan, Pakistan, uwezo wake wa kupambana na wapiganaji na kuimarisha uhusiano wa nchi hiyo na Marekani, kama sehemu ya kuunga mkono mabadilio ya kisiasa na kiuchumi.

Wakati ikiwa imebaki wiki tu kufanyika kwa mkutano huo wa kimataifa mjini London tayari baadhi ya nchi zimezindua miakati yao kwa Afghanistan.

Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani Hilary Clinton jana alizindua mikakati ya m ya muda mrefu isiyo ya kijeshi katika kuiimarisha Afghanistan na Pakistan, mkakati ambao kupelekwa kwa wataalamu wengi wa masuala ya kiraia katika eneo hilo.

Naye Waziri wa Ulinzi wa Marekani Robert Gates yuko ziarani nchini Afghanistan, kuweka sawa mambo, kabla ya kufanyika kwa mkutano huo utakaoizungumzia Afghnaistan, uliopangwa kufanyika Januari 28, mjini London.

Katika kutilia mkazo umuhimu wa amani nchini Afghanistan katika kanda hiyo, na umuhimu katika kupambana na wapiganaji, awali, Waziri Gates alisema anaamini kuwa Operesheni inayoendelea ambayo iko chini ya Al Qaeda, pamoja na vikundi vingine vya wapiganaji inalenga kudhoofisha eneo hilo.


Wakati huohuo Waziri wa mambo ya nchi za Nje wa Uingereza David Miliband amesema anatarajia kwamba nchi zitakazoshiriki katika mkutano huo wa London zitatumia nafasi hiyo kutangaza ahadi zao mpya.

Mawaziri kutoka zaidi ya nchi 60 wanatarajia kuhudhuria mkutano huo wa kimataifa wa London unaozungumzia Afghanistan.

Mkutano huo ambao pia utahudhuriwa na Rais wa Afghanistan Hamid Karzai, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon na Katibu Mkuiu wa Jumuia ya Kujihami ya NATO Anders Fogh Rasmussen unataka pia kuchochea juhudi za kuimarisha mataifa yanayokabiliwa na vita na kulizuia kundi la Al Qaeda ama washirika wake kutumia nchi hizo kama vituo vyake.

Kikao hicho pia kitapanga ratiba ya kuhamisha majukumu ya vikosi vya kigeni katika maeneo yanayodhibiti nchini Afghanistan

Mwandishi: Halima Nyanza(dpa, reuters)

Mhariri: Miraji Othman