1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maduro achukua udhibiti wa bunge Venezuela

Amina Mjahid
7 Desemba 2020

Rais wa Venezuela Nicolas Maduro ameshinda udhibiti kamili wa bunge, kufuatia uchaguzi uliofanyika siku ya Jumapili. Upinzani ulisusia uchaguzi huo na kusema uliwakilisha "udanganyifu."

https://p.dw.com/p/3mJmy
Venezuela | Parlamentswahlen PK Nicolas Maduro
Picha: Fausto Torrealba/REUTERS

Uchaguzi huo uliokosolewa na waangalizi wa kimataifa ulikuwa na idadi ndogo ya wapiga kura ya takriban asilimia 31.

Chama cha Rais Maduro cha kisoshalisti kilipata asilimia 68. Bunge ndio taasisi ya mwisho ya serikali ambayo Maduro hakuwa na udhibiti kamili nayo. Upinzani ambao idadi yao ndogo ilishiriki uchaguzi licha ya miito ya kuususia ulipata asilimia 18 ya kura.

Indira Alfonzo, Rais wa Baraza la kitaifa la uchaguzi nchini humo amesema chama hicho tawala cha muungano wa kisoshalisti na chama vyama shirika vilipata asilimia 67 ya viti bungeni.

Soma pia: Guaido aliomba jeshi kususia uchaguzi Venezuela

Hata hivyo waangalizi wa kura wa Kimataifa kama Umoja wa Ulaya na Mashirika ya majimbo ya Marekani zilikataa kutuma waangalizi wake katika uchaguzi huo uliofanyika siku ya Jumapili zikisema mazingira ya kufanyika mchakato wa kidemokrasia katika uchaguzi sio mazuri kwa sasa nchini Venezuela.

 Uchaguzi wa bunge nchini Venezuela ulifanyika 06.12.2020
Uchaguzi wa bunge nchini Venezuela ulifanyika 06.12.2020Picha: dpa/picture alliance

Kiongozi wa upinzani na mpinzani wa Maduro Juan Guaido amesema uchaguzi ulikuwa wa udanganyifu, akizungumzia idadi ndogo ya watu waliojitokeza kupiga kura. Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo ameukosoa uchaguzi huo akiuita wa ulaghai na uliopangwa na Maduro. Pompeo aliandika katika ukurasa wake wa Twitter kwamba kile kilichotokea ni udanganyifu na wala sio uchaguzi.

Nicholas Maduro aendelea kuwepo madarakani licha ya shinikizo za kidiplomasia

Kando na kupata uungwaji mkono wa Marekani pamoja na mataifa mengine 50 duniani, Guaido pamoja na serikali yake ya mpito hajafanikiwa kumuondoa Maduro madarakani au hata kulishawishi jeshi kubadilisha msimamo na kumuunga mkono.

Kiongozi wa upinzani Juan Guaido adai uchaguzi huo ulikumbwa na udanganyifu
Kiongozi wa upinzani Juan Guaido adai uchaguzi huo ulikumbwa na udanganyifuPicha: Leo Alvarez/Prensa Presidencia Guaido

Licha ya Kampeni inayofanywa na serikali ya rais Donald Trump ya kuiwekea Venezuela vikwazo na shinikizo za kidiplomasia, Maduro amebakia madarakani akiungwa mkono na jeshi la nchi hiyo pamoja na Urusi, Cuba, China na Iran.

Uchaguzi wa bunge uliofanyika hapo jana unakuja wakati Venezuela ikizidi kudidimia katika mgogoro wa kisiasa na kiuchumi. Uchaguzi huu pia unafanyika katikati ya janga la dunia la virusi vya corona, ukosefu wa nishati ya gesi nchini humo, chakula na madawa. Takriban Wavenezuela milioni 5 wamekwishaitoroka nchi hiyo.

Shirika la kimataifa la fedha duniani IMF limekadiria upungufu wa asilimia 25 mwaka huu katika mapato ya kitaifa ya Venezuela.

(EFE, AP, Reuters, AFP)