1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini

Hamidou, Oumilkher15 Aprili 2008

Uchaguzi wa Italy na matokeo yake

https://p.dw.com/p/DiB9
Waziri mkuu mteule wa Italy Silvio BerlusconiPicha: AP



Kujiuzulu waziri mkuu wa jimbo la Sachsen Georg Milbradt,maridhiano ndani ya chama cha Social Democratic kuhusu kubinafsishwa shirika la usafiri wa reli na uchaguzi nchini Italy ndizo mada zilizochambuliwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.



Tuanzie lakini Italy ambako kiongozi wa zamani wa serikali Silvio Berlusconi amebahatika kwa mara ya tatu kuchaguliwa kuwa waziri mkuu.Gazeti la SÜDDEUTSCHE ZEITUNG linaiangalia hali hiyo ifuatavyo:


Wataliana wanapenda sana ubwana na mzaha.Silvio Berlusconi ana sifa zote hizo mbili.Wengi wamempigia kura,mtu anaweza kusema kwasababu ya ufidhuli tuu,bila ya kujali ila na kero  litakalosababishwa na uamuzi wao katika daraja ya kimataifa.Wanamfuata Berlusconi wakijidanganya wenyewe, mfano wa mtu anaetembelea sarakasi akiamini kinachofanywa na mchawi ni kweli.Bila shaka hali hiyo haiwezi kudumu muda mrefu.Ingawa Berlusconi ameahidi katika kampeni za uchaguzi atatia njiani mageuzi nchini.Lakini maarifa yameonyesha,Berlusconi haaminiki.Kwa hivyo watu hawatakosea watakaposema Italy imeshindwa ."


Hayo ni maoni ya SÜDDEUTSCHE ZEITUNG la mjini München.Gazeti la HAMBURGER ABENDBLATT linamulika hali hali ya siku za mbele ya Italy na kuandika:


 Hakuna hata mmoja anaeamini kwamba tajiri huyo mkubwa kupita kiasi,ataweka kando faida za kibinafsi na kutanguliza mbele masilahi ya jamii-seuze kuachilia mbali madaraka aliyo nayo katika kudhibiti vyombo vya habari.Mwaka 2004 shirika moja la kimarekani lilipokua likitathmini uhuru wa vyombo vya habari nchini Italy,lilizungumzia juu ya "nusu uhuru tuu"-hali inayotoa onyo la kisiasa.Awamu ya tatu ya mwanasiasa huyo anaependa kujinata kua amejaaliwa,shabiki mkubwa wa mfashiti wa zamani Mussolini ni ishara ya matakiwa ya wataliana ya kumpata kiongozi shujaa katika enzi hizi za vurugu la utandawazi na mengineyo.Kwa upande mwengine lakini ushindi wake ni ishara ya mzozo wa kina wa kisiasa na kijamii katika nchi hiyo adhimu.


Na gazeti la FINCIAL TIMES DEUTSCHLAND  linaandika:


"Berlusconi na kundi lake si chochote si lolote isipokua watu wanaotaka kujifaidisha tuu.Hana azma wala nia ya kutaka kuifanyia mageuzi nchi hiyo.Inasikitisha sioo tuu kwa Italy ,bali kwa Ulaya nzima.Umoja wa ulaya haustahiki kufumba macho unapoona mmojwapo wa wanachama wake muhimu,ambae pia ni mwanachama wa jumuia ya mataifa tajiri kiviwanda,inazama kiuchumi hata katika wakati wa ukuaji wa kiuchumi ulimwenguni.Tarakimu duni za ukuaji wa kiuchumi na nakisi iliyokithiri zitadhuru soko la pamoja na sarafu ya pamoja ya Yuro.Mageuzi yanayohitajika ili kupunguza makali ya athari hizo,Berlusconi,hatosubutu hata wakati mmoja kuyatia njiani."