1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Je, nini hatma ya Trump baada ya hukumu ya mahakama?

22 Desemba 2023

Mahakama ya juu ya jimbo la Colorado nchini Marekani imetoa hukumu kwamba rais wa zamani wa nchi hiyo Donald Trump hana tena sifa za kuwania urais kwa sababu ya kuhusika kwake katika uvamizi wa bunge wa Januari 6, 2021.

https://p.dw.com/p/4aOhn
Donald Trump alipojitokeza mahakamani huko New York.
Donald Trump, Rais wa zamani wa Marekani ambaye mahakama ya Colorado imetoa hukumu kwamba hana tena sifa tena za kuwania urais nchini humo.Picha: Andrea Renault/ZUMA/picture alliance

Mahakama ya juu ya jimbo la Colorado nchini Marekani imetoa hukumu kwamba rais wa zamani wa nchi hiyo Donald Trump hana tena sifa za kuwania Urais kwa sababu ya kuhusika kwake katika uvamizi wa Januari 6, 2021 kwenye makao makuu ya bunge la Marekani, Capitol, mjini Washington DC.

Soma zaidi: Baraza la Usalama la UN laahirisha kura juu ya azimio la kusitisha mapigano Gaza

Mahakama hiyo imezuia jina la Donald Trump kuwepo kwenye orodha ya kupigiwa kura ya kuwania urais wa Marekani katika uchaguzi wa mwaka 2024 katika jimbo hilo.

Uamuzi huo wa kisheria ambao tume ya kampeni ya Trump imesema itakata rufaa kuupinga umelaaniwa vikali na chama chake cha Republican ambacho kimesema kuwa kitachukua hatua zaidi kwa kile walichokiita ni unyanyasaji wa kisiasa.

Uamuzi huo ni hatua ya kwanza.

Hukumu hii ambayo inahusu tu uchanguzi wa mchujo katika jimbo hilo la Colorado ni hatua ya kwanza kati ya nyingine kadhaa za kisheria kote nchini Marekani ikiwa ni hatua ya kutekeleza marekebisho ya marekebisho ya katiba ya 14 ya nchi hiyo inayomzuia mtu yeyote kurejea tena madarakani mtu aliyeapa kuilinda katiba ya Marekani na kisha akajihusisha na uasi.

Soma zaidi: Finland yaimarisha uhusiano wa kijeshi na Marekani kufuatia onyo la Putin

Mahakama hiyo ya Colorado imesema kuwa marekebisho hayo ya katibaya Marekani yanacho kifungo kinachomzuia Trump kuwania tena Urais na kwamba mahakama nyingi zinashikilia msimamo huo kuwa Rais Trump hastahili kushika wadhifa wa Urais kwa mara nyingine.  

Colorado/ USA
Mahakama ya juu jimboni Colorado nchini Marekani imetoa hukumu kuwa Donald Trump hana sifa za kuwania tena urais nchini humo.Picha: David Zalubowski/AP Photo/picture alliance

Mahakama hiyo imeongeza kuwa kumrejesha Trump katika orodha ya wanaowania urais wa Marekani itakuwa ni kitendo kisicho sahihi chini ya Kanuni ya Uchaguzi kwa Katibu wa Jimbo la Colorado.

Baadhi ya wapinzani wa Trump katika kinyang'anyiro cha kupeperusha bendera ya chama cha Republican katika uchaguzi ujao, wameukarisha uamuzi huo wa mahakama, mmoja akiwa balozi wa zamani wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Nikki Halle.

Nikki Halle amesema:"Sidhani kwamba Donald Trump anahitaji kuwa rais. Nadhani nahitaji kuwa rais. Nadhani hiyo ni nzuri kwa nchi. Lakini nitamshinda wazi wazi. Hatuhitaji majaji kufanya maamuzi haya.

Hata hivyo,Ron DeSantis ambaye pia anawania dhidi ya Trump katika chama cha Republican katika uchaguzi ujao ameandika katika mtandao wa X kuwa mahakama ya juu ya Marekani inapaswa kuubatilisha uamuzi huo wa mahakama ya Colorado.

Marekani I  Donald Trump
Rais wa Zamani wa Marekani Donald Trump bado anakabiliwa na mashtaka ya kuongoza njama za udanganyifu wa uchaguzi wa mwaka 2020 katika jimbo la Georgia.Picha: Joe Raedle/AFP/Getty Images

Uamuzi wa awali wa mahakama ya mwanzo uligundua kuwa ingawa Trump aliunga mkono ghasia za Januari 6, ofisi ya rais haikujumuishwa katika orodha ya nyadhifa za serikali kuu zilizoathiriwa na Marekebisho ya katiba mpya ya 14 ya nchi hiyo.

Wadau: Ni hatua muhimu kwa demokrasia ya Marekani.

 Kupitia mitandao ya kijamii, Kikundi cha kampeni cha Noah Bookbinder huko Washington kinachosimamia uwajibikaji na kufuatwa kwa sheria na ambacho ndicho kilichoipeleka kesi hiyo mahakamani kimeupongeza uamuzi huo wa mahakama na kwamba ni hatua muhimu kwa demokrasia ya Marekani.

Soma zaidi: Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin azuru Israel kujadili vita vyake Gaza.

Kwa upande wake msemaji wa kampeni wa Donald Trump, steven Cheung hawakubaliani na maamuzi hayo na kwamba watakata rufaa huku akiishutumu mahakama hiyo kwa kile alichokiita ni mpango wa kukibeba chama cha Democrat.

 Donald trump anakabiliwa pia na mashtaka ya kihistoria  kwa madai ya kuongoza njama za udanganyifu wa uchaguzi wa mwaka 2020 katika jimbo la Georgia ambapo bado upo mjadala mkali wa kisheria juu ya kama anastahili tena kurejea kuwania urais.

Hatua ya mahakama ya Colorado ni mojawapo ya kesi nyingi zinazomhusu Trump zinazoendelea kote nchini Marekani,  Mahakama kuu ya Minnesota ilitupilia mbali hatua kama hiyo mwezi uliopita.